SERIKALI kupitia Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) inatarajiwa kutumia zaidi ya Sh bilioni saba katika ujenzi wa daraja jipya la Berega wilayani Kilosa, Morogoro. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Hayo yamebainishwa leo tarehe 22 Februari 2023 na Mwenyekiti wa Bodi hiyo Mhandisi Florian Kabaka katika ziara ya ukaguzi wa Miradi iliyofanywa na Bodi ya Ushauri ya TARURA Mkoani Morogoro.
Alisema ujenzi wa daraja hilo utaleta manufaa makubwa kwa wananchi wa Berega na maeneo mengine waliyokuwa wakipata tabu baada ya daraja la awali kuvunjika.
“Daraja hili linagharimu zaidi ya Sh bilioni saba na ni moja kati ya madaraja makubwa kabisa ambayo TARURA inatekeleza ujenzi wake kwa kutumia fedha za tozo. Sisi kama Bodi tunaridhika na namna mradi unavyoendelea ambapo tunaambiwa umefikia asilimia 72 na unatarajia kukamilika mwezi Juni, 2023, “ alisema Mhandisi Kabaka.
Aidha, alieleza daraja hilo litaleta ukombozi mkubwa kwa wananchi wa Berega kwa sababu litawaunganisha na maeneo mengine kama Gairo, Dodoma na Tanga, pamoja na kuwarahisishia wananchi kufika Hospitali ya Wilaya ya Berega.
Naye Kaimu meneja wa TARURA, mkoa wa Morogoro Mhandisi Benjamini Maziku, alisema daraja hilo litakapokamilika litakuwa ni ukombozi mkubwa kwa wananchi Berega na Wilaya ya jirani ya Kilindi kwa sababu litakuwa na uwezo wa kupitisha magari ya aina yote hivyo kuwarahisishia usafiri na usafirishaji wa mazao.
“Tunamshukuru Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kutupatia fedha hizi za tozo kwa ajili ya kuwa hudumia wananchi hawa, sisi kama TARURA mkoa, tusingeweza kujenga daraja hili ambapo takribani bilioni 7.9 zitatumika.
“Hapo awali kabla ya kuongezewa bajeti na hasa fedha hizi za tozo, hii ndiyo ilikuwa bajeti ya mkoa mzima, sasa bajeti ya mkoa imeongezeka mpaka Sh bilioni 26. Tunamshukuru sana Rais, “ alisema Maziku.
Kwa upande wake, Michael Majoro, mkazi wa Berega alisema kukamilika kwa ujenzi wa daraja hilo itakuwa ni faraja kubwa kwao Kwani itawaondolea matatizo mengi yaliyokuwa yakiwakabili hasa nyakati za mvua.
“Kwakweli tunamshukuru Rais Samia kwa kutujengea daraja hili, hapa wapo waliokufa, mifugo kusombwa na maji, wamama kujifungulia ng’ambo ya pili kutokana na kushindwa kuvuka wakati hospitali ipo hapo karibu tu. Mheshimiwa hapa ametukomboa kwakweli tunaona hili ni daraja la kisasa kabisa na lipo juu,” Majoro.
Mradi wa ujenzi wa daraja la Berega unahusisha ujenzi wa daraja lenye urefu wa mita 140, barabara mkaribio za daraja mita 600 na maboresho ya barabara kutoka Berega kwenda Dumbalume kilomita saba katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa.
Bodi ya TARURA inaendelea na ziara yake ya ukaguzi wa miradi mbalimbali inayotekelezwa na TARURA katika mikoa ya Morogoro, Pwani na Dar es Salaam.
Leave a comment