SERIKALI ya Tanzania, imetumia zaidi ya Sh.60 bilioni kugharamia miradi ya mbalimbali ya maendeleo Manispaa ya Moshi Mkoa wa Kilimanjaro. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Kiasi hicho cha fedha ni kuanzia mwaka 2015-2020 wa Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais John Pombe Magufuli, ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Baadhi ya miradi hiyo ni kuweka taa za barabarabi Moshi Mjini na ujenzi wa Stendi Kuu ya Kimataifa ya Mabasi ya Mikoani eneo la Ngangamfumuni nje kidogo ya Mji wa Moshi.
Ujenzi wa stendi unafanywa na kampuni ya CRJE (East Africa) ulianza mwaka 2019 na ulitarajiwa kukamilika mwaka 2021.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Manispaa ya Moshi, Mkoa wa Kilimanjaro, Michael Mwandezi alipokuwa akizungumza na katika Mahojiano na Amsha Amsha 2020 ya Uhuru FM.
Mwandezi amesema, stendi hiyo itakapokamilika itakuwa na uwezo wa kupaki magari madogo 300 na uwezo wa kuchukua mabasi 70 kwa wakati mmoja.
Pia, ujenzi huo amesema umechochea ajira zaidi ya 10,000E ambapo kati ya hizo zipo ajira za muda mfupi na mrefu ambazo ni 400.
“Niwaambieni tu kuwa mradi huu wa Stendi ya Moshi utakuwa mkubwa nchini na utauzidi pia ule wa Mbezi Mwisho Jijini Dar es salaam” amesema Mwandezi
Amesema, jengo lake litakuwa na ghorofa mbili, kutakuwa na Hotel na maduka makubwa na kwamba mkandarasi wa ujenzi huo ndiye aliyejenga Daraja la Kigamboni Jijini Dar es salaam.
Mwandezi amesema, jengo la standi hiyo kuu litakuwa pia na ofisi za Kimataifa za Uhamiaji.
Miradi mingine iliyotekeleza katika Manispaa ya Moshi ni pamoja na mradi wa Dampo la kisasa la Mtakuja lililopo kilometa 15 kutoka Moshi Mjini hadi eneo la Mtakuja.
Amesema fedha hizo pia zimetumika kujenga zaidi ya kilomita 16 za barabara kwa kiwango cha na taa za barabarani Mjini Moshi.
Kwa upande wake, Mhandisi wa Manispaa hiyo, Richard Sanga amesema mradi huo wa Dampo unatekelezwa na kampuni ya Rocktonic na kwamba zaidi ya Sh.2 bilioni zimetumika katika ujenzi wake.
Mhandishi Sanga amesema, eneo la mradi huo lina ukumbwa wa hekari 15 na ndani ya mradi huo kutajengwa Kiwanda cha mbolea kinachotokana na takataka zinazotupwa katika Dampo hilo.
“Tayari mashine kwa ajili ya Kiwanda cha Mbolea zimeshanunuliwa na zinasubiriwa kufungwa na wananchi watanufaika na Mbolea inayotokana na mabaki ya chakula,” amesema
“Wananchi waliopo jirani, watanufaika na Dampo hilo, hivyo waanze kuleta taka zao hapa na takataka zitakazotupwa hapo ni zile zisizooza,” amesema Sanga
Aidha Mhandisi Sanga amesema, tayari elimu kwa wananchi wameshaanza kupewa kuhusu namna ya kutunza taka zinazooza kwa manufaa ya kuzipeleka ili zikatengenezwe Mbolea.
Pia amesema Dampo hilo la kisasa limetengezezwa kisasa hata Mvua ikinyesha halitajaa kwani kuna chemba za kupitisha maji zimejengwa chini li kuruhusu maji kutoka nje.
Katika kulinda mazingira chini ya Dampo hilo umewekwa naironi ili kutoharibu mazingira.
Katika hatua nyingine, serikali ya awamu ya tano, imepeleka Shule ya sekondari ya Ufundi Moshi, Sh.2 bilioni kwa ajili ya ukarabati wa shule hiyo kongwe inayofundisha pia masuala ya Ufundi kwa wanafunzi wa kidato cha nne na sita.
Mkuu wa Shule hiyo, Erasmus Kyara amesema shule hiyo ipo kata ya karanga na ni miongoni mwa shule kongwe zilizokarabatiwa na serikali.
“Shule hii ilianzishwa mwaka 1957 na Mimi mwalimu Kyara ni mwalimu wa 17 kuwa mkuu wa shule hiyo tangu kuanza kwake,” amesema Kyara
Amesema ukarabati katika shule hiyo umehusisha jengo la utawala, mabweni 40 ya wavulana na bweni moja la wasichana, madarasa matatu, maabara pamoja na jengo la maktaba yenye uwezo wa kuchukua watu 200 na ukarabati wa majiko.
Leave a comment