Katika kuhakikisha usafiri wa majini unaimarika, serikali imetenga kiais cha Sh. bilioni 5 katika bajeti ya mwaka huu kwa ajili ya ukarabati na kununua vivuko pindi inapohitajika. Anaripoti Moses Mseti, Mwanza… (endelea)
Imesema pia imetenga Sh. milioni 50 kwa ajili ya ukarabati wa kivuko cha MV Nyerere kilichopinduka Septemba 20 mwaka jana wakati kikisafirisha abiria kutoka Bugorola kwenda Ukara wilayani Ukerewe na kusababisha abiria 230 kufariki na wengine 41 kuokolewa.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme nchini (Temesa), Mhandisi Japhet Masele amesema kama wakala wametenga Sh bilioni 5 ambazo ni mapato ya ndani za kukarabati vivuko.
Mhandisi Masele amesema pamoja na fedha za ndani, pia Serikali kuu imekuwa ikitoa fedha kwa Temesa wakati panapojitokeza kuwapo na shughuli ya ujenzi wa kivuko kipya au ukarabati ikiwa lengo ni moja kuondoa changamoto za vyombo vya usafirishaji abiria na mizigo majini.
“Tunaposema tumetenga Sh bilioni 5 kama fedha za ndani, tayari tumepanga kutengeneza boti mbili mpya ambapo moja itapalekwa katika Kisiwa cha Ilugwa na nyingine tutaangalia palipo na uhitaji wa haraka, kama Serikali tunatambua uwepo wa vivuko unaongeza uchumi kwa wananchi.
“ vipo vivuko ambavyo vinaziunganisha nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki(EAC), mfano kivuko cha Kigongo-Busisi ambacho kwanza kinaunganisha mkoa na mkoa, pia kinatumiwa na nchi za nje.Vile vile kivuko cha Rusumo nacho kinatumika kwa EAC ambapo vyote vinavusha malori ya mafuta,”alisema.
Pia Mhandisi Masele amesema Serikali muda wowote itasaini mkataba wa ujenzi wa kivuko cha kipya cha Bugorola-Ukara ambacho kitakuwa mbadala wa MV Nyerere iliyopinduka Septemba 20, mwaka jana na kusababisha vifo.
Leave a comment