SERIKALI ya Tanzania imesema, Sh.42.3 bilioni zimetengwa ili kulipa fidia kwa wananchi waliopisha miradi wa kusafirisha umeme kutoka Kinyerezi na Bwawa la Mwalimu Nyerere. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Kauli hiyo, imetolewa leo Jumatatu tarehe 19 Aprili 2021, bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Nishati, Stephen Byabato wakati akijibu swali la Ridhiwan Kikwete, Mbunge wa Chalinze kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).
“Je, ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi wa Chalinze waliopisha ujenzi wa miundombinu ya miradi ya kusafirisha umeme kutoka Kinyerezi na Bwawa la Mwalimu Nyerere,” ameuliza Ridhiwani
Akijibu swali hilo, Byabato amesema, Serikali kupitia Tanesco, inatekeleza mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovolti 400 kutoka kituo cha kuzalisha umeme cha Julius Nyerere hadi Chalinze na ujenzi wa kituo cha kupoza umeme katika Kijiji cha Chaua – Chalinze.
Amesema, Serikali kupitia Tanesco, imekamilisha tathimini ya mali za wananchi na taasisi zilizopisha utekelezaji wa mradi huu na fidia kuidhinishwa na mthamini mkuu wa Serikali.
Naibu waziri huyo amesema, jumla ya Sh.42.3 bilioni, zimetengwa katika bajeti ya mwaka 2021/22, kwa ajili ya malipo ya fidia kwa wananchi waliopisha mradi.
Amesema, fidia ya wananchi hao itaanza kulipwa kuanzia Mwaka wa fedha2021/22 baada ya taratibu zote kukamilika.
Leave a comment