UJENZI wa kituo kipya cha Mabasi cha Ubungo kinachotarajiwa kujengwa maeneo ya Mbezi Luis kinakadiliwa kutumia Sh. 28.72 bilioni, anaandika Dany Tibason.
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, Selemani Jafo amesema gharama za ujenzi wa kituo hicho zimekadiriwa kuwa Sh. 28.71 bilioni zitazotolewa kwa ushirikiano wa Halmashauri ya Jiji na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa Serikali za Mitaa (LAPF).
Jafo alitoa maelezo hayo bungeni akijibu swali la Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea (Chadema) alitaka kujua serikali imefikia hatua gani katika kutekeleza ahadi katika utekelezaji wa kuhamisha kituo cha mabasi cha Ubungo.
“Serikali ilihaidi kuhamisha kituo cha mabasi cha Ubungo kukipeleka eneo la Mbezi jimbo la Kibamba lakini mpaka sasa jambo hilo halijatekelezwa.
“Je serikali imefikia hatua gani katika kutekeleza ahadi hiyo, Je mradi huo wa kuhamisha kituo cha mabasi unatarajia kutumia kiasi gani cha fedha,” alihoji Kubenea.
Jafo amesema hadi sasa tayari Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kwa kushirikiana na wameanzisha kampuni ya ubia ya Mzizima Properties Limited ambayo itahusika na usimamizi na uendeshaji wa shughuli za kituo cha Mabasi cha Ubungo (UBT) kila siku.
Amesema kazi inayoendelea ni kumtafuta mtaalam mshauri kwa ajili ya kuthibitisha usanifu wa mwisho wa kina wa mradi ili kumpata mkandarasi wa ujenzi wa mradi.
Aidha amesema gharama halisi zitajulikana baada ya usanifu wa kina utakaofanywa na mtaalam mshauri.
Leave a comment