MAHAKAMA Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Dar es Salaam, imepiga marufuku watu wanaohudhuria mahakamani hapo bila kuvaa barakoa. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Agizo hilo limetolewa leo Jumatano, tarehe 15 Desemba 2021 na Naibu Msajili wa mahakama hiyo, Magdalena Ntandu, akitangaza utaratibu huo kwa wanachama na wafuasi wa Chama cha Chadema, waliohudhuria kusikiliza kesi inayomkabili mwenyekiti wao, Freeman Mbowe na wenzake watatu.
Ntandu amesema kuwa, kuanzia kesho Alhamisi, tarehe 16 Desemba 2021, mtu asiyevaa barakoa hataruhusiwa kuingia mahakamani hapo kwa ajili ya kusikiliza kesi.
Amesema agizo hilo linalenga kujikinga dhidi ya maambukizi ya Ugonjwa wa Virusi vya Korona (UVIKO-19).
“Kuanzia kesho tuvae barakoa, tunawe mikono, nawasisitiza hilo mvae barakoa kama mtu hajavaa barakoa haruhusiwi kuingia ndani na tusingependa litokee hili. Kesho usipovaa barakoa tukikutoa usilalamike,” amesema Ntandu.
Mbali na agizo hilo, Ntandu amewahimiza watu wanaohudhuria mahakamani hapo, kufuata ushauri unaotolewa na watalaamu wa afya katika kudhibiti maambukizi ya ugonjwa huo, ikiwemo kunawa mikono na kukaa umbali wa mita moja baina ya mtu na mtu.
Mbali na Mbowe, washtakiwa wengine katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi, ni waliokuwa makomandoo wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Halfan Bwire Hassan, Adam Kasekwa na Mohammed Ling’wenya.
Kesi hiyo yenye mashtaka ya ugaidi, inasikilizwa mfululizo mbele ya Jaji Joachim Tiganga, ambapo upande wa jamhuri unaendelea kutoa ushahidi wake.
Leave a comment