SERIKALI imeeleza itatumia Dola za Marekani milioni 120 (Sh. 278.8 Bil), kwa ajili ya kutatua changamoto ya mafuriko yanayotokana na Bonde la Mto Msimbazi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Alhamisi tarehe 29 Aprili 2021, bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais – Muungano na Mazingira, Hamad Chande wakati akijibu swali la Mbunge wa Kinondoni, Abass Tarimba.
Chande amesema, Dola 100 milioni ni fedha za ufadhili kutoka Shirika la Kimataifa la Manedeleo la Uingereza (DFID), kupitia mradi wa kukabiliana na athari zitokanazo na mabadiliko ya tabia ya nchi.
Huku dola 20 Mil. zikiwa ni fedha za mkopo nafuu kutoka Benki ya Dunia (WB), kupitia Mradi wa Uendelezaji Mkoa wa Dar es Salaam (DMDP).
“Ofisi ya Rais -TAMISEMI inatekelza mradi wa DMDP kwa mkopo nafuu wa Dola za Marekani 300 milioni kutoka WB, aidha, serikali kwa ufadhiri wa DFID inatekelza programu ya kusaidia halmashauri na Serikali Kuu kukabiliana na athari zitokanazo na mabadiliko ya tabia ya nchi.
“Programu hii itaanza kutatua changamoto inazokabili Bonde la Mto Msimbazi. Tayari DFID imeshatenga dola 20 milioni kwa ajili ya Bonde Msimbazi, WB kupitia madi wa DMDP, imekubali kutoa mkopo wa nyongeza Dola 100 Mil kwa ajili ya kukabiliana na changamoto za Msimbazi,” amesema.
Katika swali lake la msingi, Tarimba alihoji lini serikali itaanza ujenzi wa Mto Msimbazi, ili kuondoa changamoto ya mafuriko inayowakumba wakazi wa jimbo lake hasa Kata za Kigogo, Mzimuni na Magomeni.
Ambapo Chande alijibu, kwamba serikali imepanga kubadili eneo la bonde hilo ili liwe la uwekezaji na fursa mbalimbali.
“Ili kufikia azma hiyo, usanifu wa mradi huo umekamilika , utekelezaji wa mradi utaanza baada ya kupata idhini ya serikali kuhusu matumizi ya fedha hizo za mkpo kupitia Wizara ya fedha na Mipango,” amesema Chande.
Leave a comment