SERIKALI imepokea gawio la kiasi cha Sh. 21.8 bilioni, kutoka benki ya makabwela – National Microfinance Bank (NMB) – ikiwa ni sehemu ya faida ya Sh. 206 bilioni 206, iliyopatikana katika benki hiyo kwa mwaka uliyopita. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Akipokea mfano wa hundi yenye thamani ya kiasi hicho cha fedha, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano, Dk. Philip Mpango amesema, serikali inathamini mchango wa benki hiyo katika maendeleo ya taifa.
Ameupongeza uongozi wa benki hiyo kwa jitihada zake mbalimbali katika kuchangia uchumi wa nchi na wananchi mmoja mmoja.
Tayari fedha hizo zimeshaingizwa serikalini, kupitia akaunti ya Msajili wa Hazina.
Dk. Mpango ameelekeza mabenki pamoja na taasisi nyingine za fedha, kutumia utaalamu na uzoefu walionao katika sekta hiyo, kutafuta suluhisho la kuondokana na mzigo wa riba, wanaotozwa wananchi wakati wa kuchukua mikopo na kuweka amana katika taasisi hizo.
Aidha, Dk. Mpango amezielekeza taasisi nyingine ambazo serikali ina hisa, kujiendesha kwa ufanisi ili ziweze kutoa gawio serikalini.

Amesema, fedha hizo zinahitajika ili kusaidia utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuonya kuwa taasisi ambazo zitashindwa kujiendesha, watendaji wake wataondolewa kwenye nafasi zao.
Katika hatua nyingine, Dk. Mpango amempongeza Msajilli wa Hazina, Athumani Mbuttuka kwa usimamizi wa mashirika ya umma, taasisi pamoja na kampuni 287 yanayoweza serikali kupata gawio kulingana na uwekezaji wa hisa na umiliki wa moja kwa moja.
Akizungumza kwenye hafla hiyo, mwenyekiti wa Bodi ya NMB, Dk. Edwin Mhede alisema, katika mwaka wa fedha wa 2019, benki yake iliipatia serikali gawio la Sh. 15.2 bilioni.
Alisema, kuongezeka kwa gawio hilo, kunatokana na maelekezo ya Dk. Mpango, wakati akiwa waziri wa fedha, ambapo aliiagiza benki hiyo kuongeza gawio kwa kuboresha huduma zake.
Alisema, agizo la Dk. Mpango lilichagiza, benki hiyo kupata faida kubwa ya kuiwezsha kutoa gawio hilo la Sh. 21.8 bilioni, sawa na ongezeko la 43 asilimia.
Aliahidi kuwa mwaka ujao tutaongeza ubunifu na uwajibikaji zaidi na kuongeza gawio kubwa zaidi serikalini.
Naye afisa mtendaji mkuu wa NMB, Ruth Zaipuna, ameipongeza serikali kwa kuendelea kuweka mazingira wezeshi ya kufanya biashara nchini ambayo yamechochea mafanikio ya benki hiyo na kuweza kufikisha mtaji wa Sh. 11 trilioni.
Zaipuna alibainisha kuwa pamoja na kutoa gawio hilo, Benki yake pia imelipa kodi mbalimbali serikalini zenye thamani ya Sh. 245 bilioni.
Ameeleza pia kuwa kiasi cha Sh. 1.4 bilioni, kimetumika katika kuwezesha sekta za elimu, afya, kupitia mpango utoaji wa huduma kwa jamii.
Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Fedha na Mipango, Mwigulu Nchemba, ameupongeza uongozi wa NMB kwa kusimamia utendaji wa benki hiyo na kufanikisha kupatikana faida.
Ameagiza kuendelea kudhibiti matumizi, kuongeza mapato na kusimamia vyema mikopo.
Amemtaka Msajili wa Hazina kuendelea na juhudi za kusimamia taasisi na mashirika ya umma kwa kuwa ufanisi wa mashirika hayo una faida kwa serikali.
Akijibu maelezo hayo, Msajili wa Hazina, amewapongeza wafanyakazi wa ofisi yake kwa usimamizi mzuri wa kazi, jambo lililosababisha kuongezeka kwa maduhuli ya serikali kutoka Sh. 225.467 bilioni, mwaka 2015/16 hadi Sh. 753.95 bilioni mwaka 2019/20.
Amesema, ongezeko hilo, ni asilimia 77 na fedha hizo, ambazo ziliingizwa moja kwa moja katika akaunti ya Msajili wa Hazina.
Leave a comment