SEKTA ya afya ni sekta muhimu kwa maendeleo ya jamii na kwa kulitambua hilio, Benki ya NMB imeshirikiana na Serikali kupitia Wizara ya Afya kuboresha huduma za Afya kwa Wilaya ya Arusha kwa kutoa msaada wa vifaa tiba vyenye jumla ya thamani ya zaidi ya Sh. milioni 26 katika kituo vya Afya – Mkonoo. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Vifaa tiba hivyo vilivyotolewa ni vitanda 10 vya kujifungulia kwa kina mama pamoja na vitanda 10 vya kulaza wagonjwa wa kawaida.
Aidha, katika Kituo cha Afya Levolosi waliwakabidhi mabenchi 20 ya kusubiri huduma na kukalia kwa wasindikizaji.
Kabla ya kukabidhi vifaa hivyo, Afisa Mkuu wa Huduma Shirikishi wa NMB, Nenyuata Mejooli alisema vifaa hivyo ni moja ya ushiriki wa benki hiyo katika maendeleo ya jamii.
Alisema na NMB ni benki inayoongoza Tanzania hivyo wanao wajibu wa kuhakikisha jamii inayowazunguka inafaidika kutokana na faida wanayoipata.
Alisema Benki ya NMB imekuwa ikipokea maombi mengi ya kuchangia katika miradi ya jamii, lakini benki imejikita zaidi katika maeneo ya elimu, afya na misaada muhimu katika nyakati ngumu kama za majanga.
“Tumekuwa mstari wa mbele kuchangia huduma za kijamii kwa lengo la kurejesha sehemu ya faida yetu kwa jamii.
“Kwa zaidi ya miaka 10 mfululizo, Benki ya NMB imekuwa ikitenga asilimia moja ya faida yake kama sehemu ya uwajibikaji kwa jamii inayoizunguka,” alisema
Leave a comment