MDHAMINI Mkuu wa Ligi ya NBC , Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) leo Jumatano imezindua kombe jipya la ligi kuu ya soka ya Tanzania bara lililoboreshwa. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).

Kombe hilo ambalo limezinduliwa mbele ya waandishi wa habari jijini Dar es Salaam litakabidhiwa kwa mabingwa wa ligi kuu ya Tanzania mara kwa msimu huu na misimu ijayo.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya NBC, Mkuu wa kitengo cha Mawasiliano wa benki hiy,o Godwin Semunyu alisema benki ya NBC ikiwa kama mdhamini mkuu wa ligi imeboresha kombe kutokana na maoni ya wadau mbalimbali mbali wa soka.

“NBC ikiwa mdhamini mkuu wa ligi ya Tanzania bara inajivunia mafanikio makubwa ya ligi yetu. Kwa sasa ligi yetu ni ya tano kwa ubora Afrika nah ii ni hatua kubwa na nzuri kwa soka letu. Leo tumezindua kombe lililoboreshwa ikiwa pia ni sehemu ya kuongeza thamani kwa ligi yetu,” alisema.

Godwin aliongeza kuwa, ikiwa ni sehemu ya maboresho ya ligi, benki ya NBC inatoa bima kwa wachezaji wote wa ligi kuu pamoja na familia zao na pia mikopo ya mabasi kwa timu zinazoshiriki ligi.

“Ili kuongeza hamasa kwa wachezaji na makocha, tunatoa tuzo mbali mbali kwa makundi haya kila mwezi. Benki ya NBC itaendelea kutoa mchango wake katika kusaidia maendeleo ya michezo hapa nchni kwa kuwa inatambua umuhimu na mchango wa michezo kwa maendeleo,” aliongezea
Kwa upande wake Mkurugenzi wa fedha wa Bodi ya ligi, Ibrahim Mwayela alisema udhamini wa NBC umekuwa wenye tija kubwa kwa ligi na kuongeza kuwa NBC ni mdau mkubwa katika maendeleo ya soka hapa nchini.
‘Leo Tanzania tunajivunia ligi yetu kuwa moja katika ligi bora barani Afrika tukishikilia nafasi ya tano. Tunaishukuru sana benki yaNBC kwa udhamini wake ambao umesaidia kufika hapa tulipo huku tukisonga mbele kwa kujiamini,” alieleza.
Leave a comment