BENKI ya Taifa ya Biashara (NBC) ambayo ni mdhamini Mkuu wa Ligi Kuu ya Soka ya Tanzania Bara, (NBC Premiere League) jana tarehe 30 Aprili, 2022 iliipamba mechi ya watani wa jadi katika soka la Tanzania kati ya Yanga na Simba kwa kuandaa matukio kadhaa. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Matukio hayo yaliwalenga wapenzi wa mchezo huo pamoja na wateja wa benki hiyo ikiwemo kukabidhi tuzo na zawadi kwa mchezaji bora na kocha bora wa mwezi Machi katika ligi hiyo.
Shughuli zote hizo ziliongozwa na maofisa waandamizi wa benki hiyo wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Theobald Sabi ambaye alipata wasaa wa kukabidhi tuzo na zawadi ya fedha kiasi cha sh mil 1, kwa mchezaji wa klabu ya Simba Clatous Chama alietangazwa mchezaji bora wa ligi hiyo kwa mwezi Machi sambamba na Kocha Mkuu wa Klabu hiyo, Pablo Franco ambaye pia alitangazwa kocha kwa mwezi huo na hivyo kuzawadiwa tuzo pamoja na fedha kiasi cha sh milioni moja kutoka kwa mdhamini huyo.
Tukio hilo lililoshuhudiwa na maelfu ya mashabiki waliojitokeza kutazama mechi hiyo katika Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam, lilitanguliwa na matukio mengine ikiwemo mapokezi ya wateja wa benki hiyo kutoka mikoa mbalimbali hapa nchini waliobahatika washindi katika Droo ya Jaza Kibubu Na NBC.
Washindi hao walipata fursa ya kushuhudia mechi hiyo wakiwa wamelipiwa gharama zote ikiwemo za usafiri, malazi sambamba na kupatikiwa tiketi za VIP kwa ajili ya kushuhudia mtanange huo uliomalizika kwa sare ya bila kufungana.
Pamoja na washindi hao benki hiyo pia iliandaa mwaliko rasmi kwa ajili ya wateja wake mashuhuri wakiwemo viongozi waandamizi kutoka mashirika na taasisi mbalimbali pamoja na wadau wengine wa benki hiyo waliopata wasaa kupata chakula cha mchana pamoja na viongozi wa benki ya NBC kisha kwa pamoja walielekea Uwanja wa Taifa kushudia mechi hiyo wakiwa katika msafara maalum.
Aidha, mashabiki waliojitokeza kutazama mechi hiyo walipata fursa ya kupata huduma mbalimbali za kifedha kutoka benki ya NBC kupitia maofisa wake mbalimbali waliokuwa wakitoa huduma hizo kwenye viunga vya vya uwanja huo, hatua iliyotoa fursa kwa mamia ya mashabiki hao kujiunga na huduma za benki hiyo ikiwemo kufungua akaunti mbalimbali pamoja na kufanya mihamala ya kifedha wakiwa maeneo hayo.
Leave a comment