Benki ya Exim Tanzania imekabidhi msaada wa madawati 100 yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 20 mkoani Mbeya ikiwa ni mwendelezo wa mkakati wa benki hiyo wa kutoa msaada wa madawati 1000 katika mikoa mbalimbali hapa nchini ili kuchangia utoaji wa elimu bora kupitia mpango wake wa uwajibikaji wa Jamii (CSR) ujulikanao kama Exim Cares. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Madawati hayo yalikabidhiwa na Mkuu wa Idara ya Masoko na Mawasiliano Benki ya Exim Bw Stanley Kafu kwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Zuberi Homera wakati wa hafla fupi ya makabidhiano iliyofanyika leo tarehe 16 Machi, 2022 ofisini kwake.
Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na viongozi wengine waandamizi wa Mkoa huo akiwemo Katibu Tawala wa mkoa huo, Angelina Lutambi.
Akizungumza baada ya kupokea msaada huo Homera pamoja na kuishukuru benki ya Exim, amesema msaada huo unakwenda sambamba na jitihada za serikali za kuboresha hali ya elimu mkoani humo.
Pia msaada huo utasaidia kupunguza uhitaji wa madawati unaotokana na miradi mingi ya ujenzi wa vyumba vya madarasa inayoendelea mkoani humo.
“Msaada huu utasaidia kupunguza changamoto ya uhaba wa madawati katika baadhi ya shule zetu…tunashukuru sana wenzetu wa Benki ya Exim kwa msaada huu na tunaomba muendelee kusaidia kwenye maeneo mengine pia ikiwemo sekta ya afya.
“Mheshimiwa Rais anapambana kutafuta fedha kwa ajili ya miradi mikubwa inayoendelea nchini hivyo ni jambo linalotia moyo kwake kuona wadau kama mabenki mkiendelea kumuunga mkono,” amesema.
Akizungumza kwenye hafla hiyo Katibu Tawala wa Mkoa Mbeya, Angelina Lutambi amezitaja baadhi ya shule zitakazonifaika na msaada huo kuwa ni Shule ya Msingi Mwenge na Shule ya Msingi Jitegemee za jijini humo zinazokabiliwa na uhaba mkubwa wa madawati.
Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Masoko na Mawasiliano Benki ya Exim, Stanley Kafu amesema kuwa benki hiyo imejitolea kusaidia katika kuboresha ustawi wa jamii kupitia misaada ya kijamii ikiwemo elimu na kwamba wameguswa sana na suala la changamoto ya madawatikwenye baadhi ya maeneo hapa nchini sababu iliyosababisha wao kuchukua hatua hiyo ili kuboresha zaidi sekta hiyo muhimu.
“Ni furaha kwetu kuwa sehemu ya kutatua changamoto kwenye sekta muhimu kama hii. Huu ni mwendelezo tu bado tunaendelea na mikoa mingine kwa kuwa lengo ni kutoa msaada wa madawati 1000 kama tulivyomuahidi Mh Waziri Mkuu Kassim Majaliwa wakati tunazindua mpango huu Mkoani Mtwara mwishoni mwa mwaka jana,’’ amesema.
Kafu ameitaja mikoa mingine ambayo imenufaika na mpango huo kuwa ni Mtwara na Mwanza.
Aidha, ameshauri pia wanafunzi na walimu watakaonufaika na msaada huo kutunza madawati hayo ili yaweze kutumika kwa muda mrefu na hivyo kusaidia walengwa wengi zaidi.
Leave a comment