BENKI ya Exim Tanzania imezindua huduma mpya ya bima ya maisha iitwayo ‘Pamoja Hadi Mwisho’ mahususi kwa ajili ya vikundi rasmi na visivyo rasmi, ikilenga kuongeza ushirikishwaji wa jamii zaidi katika kupata huduma hiyo muhimu.
Bima hiyo ya maisha inayopewa amana na Kampuni ya Bima ya Alliance Life assurance itatolewa kwa vikundi rasmi na visivyo rasmi ikilenga kusadia vikundi hivyo na wanavikundi dhidi ya majanga yatokanayo na vifo, ulemavu wa kudumu na elimu kwa watoto wanaoachwa pindi mwanachama anapofariki. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Bima hiyo jijini Dar es Salaam leo tarehe 9 Mei, 2022, Mkuu wa Matawi ya Benki ya Exim, Agnes Kaganda amesema huduma hiyo inakwenda sambamba na adhma ya serikali katika kuhakikisha kwamba kila Mtanzania anafikiwa na huduma za bima.
Aidha, Kaimu Mkuu wa kitengo cha Bima cha Benki ya Exim, Melchizedeck Muro amesema “Bima hii ya maisha kwa vikundi ya ‘Pamoja Hadi Mwisho’ imeletwa kwa lengo la kuhakikisha Watanzania hawaachwi nyuma linapokuja suala la kujilinda wao,familia zao na wapendwa wao.
“Ndio maana kupitia Bima Hii tumegusa vikundi rasmi na vile visivyo rasmi ikiwemo vikundi vya wafanyakazi, Wajasiriamali, vyama vya ushirika, makundi ya mitandao ya kijamii mfano Whatsapp, Facebook, na Telegram na vikundi vingine vya namna hiyo,’’ ametaja.
Bima ya maisha ya ‘Pamoja Hadi Mwisho’ Inamlinda mwanachama na familia yake shehemu yoyote na muda wowote walipo ndani ya Tanzania.
Akizungumzia zaidi kuhusu faida za Bima hiyo, Melchizedeck Muro amesema: “Kupitia Bima hii hakutakuwa hakuna muda wa kusubiri (Waiting Period). Fao litatolewa ndani ya masaa 72 baada ya kupokea nyaraka zote za madai. Mwanachama wa bima ya ‘Pamoja Hadi Mwisho’ atanufaika yeye mwenyewe, mwenza wake, watoto (nafasi nne kwa ajili ya watoto wenye umri kuanzia miaka (0 – 21)), wazazi, na wakwe’’, ametaja.
Juma Patrice Meneja wa Bima kutoka Alliance Life Assurance ameongeza kuwa, endapo mwanachama au mtegemezi wa mwanachama (mwenza au watoto au wazazi au wakwe) atafariki kutokana na ajali au ugonjwa, mkono wa pole wa rambirambi wa kiasi cha Sh milioni 3.5 hadi Sh milioni sita au kiasi cha Sh. 500,000 hadi Sh milioni tano kitatolewa kwa familia ya mwanachama aliyefariki au kwa mwanachama aliyefiwa na mtoto au mwenza au mzazi au mkwe. Rambirambi hii itatolewa ndani ya masaa 72, baada ya kupokea nyaraka zote za madai.
Aidha, amefafanua kwamba kupitia bima hiyo ikitokea mwanachama amepata ulemavu wa kudumu unaotokana na ajali, fao la kuanzia kiasi cha Sh milioni 3.5 hadi Sh milioni sita litatolewa baada ya kupokea nyaraka zote za madai. Fao hili limegawanyika katika makundi matatu; imara, hakika na salama.
“Bima hii ya ‘Pamoja Hadi Mwisho’ inatambua umuhimu wa elimu kwa watoto. Hivyo endapo mwanachama akifariki na kuwaacha watoto wakiwa bado masomoni, familia ya mwanachama itapewa fao la kiasi cha Sh mil 1 kwa lengo la kuwawezesha Watoto hadi wanne kuendelea na masomo katika mwaka huo husika bila kukwama. Fao hili linatolewa mara moja tu’’ amebainisha.
Kwa upande wake Mkuu wa Idara ya Bima kupitia Mabenki kutoka Kampuni ya Bima ya Alliance Life Assurance Ltd., Juma Patrice amewahakikishia wateja kuwa huduma hii ni bora.
Pia inalenga kuwagusa wana jamii moja kwa moja huku akibainisha kuwa kampuni hiyo imejipanga kuhakikisha huduma hiyo inatolewa kwa kukidhi matakwa na malengo ya kuanzishwa kwake kwa vikundi pekee vinanvyoanzia watu watatu na walengwa wakiwa na umri miaka 18 – 75.
Leave a comment