MBUNGE wa Viti Maalum, Upendo Peneza (Chadema) ameitaka serikali iangalie uwezekano wa kupunguza kodi katika vifaa vya ujenzi ili wananchi waweze kujenga nyumba bora, anaandika Dany Tibason.
Pia mbunge huyo katika maswali ya nyongeza alihoji ni lini serikali itarekebisha sheria ya madini ili wale wanaopisha sehemu zenye madini ili kuhakikisha wanapatiwa madai yao stahiki bila kupunjwa.
Awali katika swali la msingi la mbunge huyo, alitaka kujua serikali ina mkakati gani kuhakikisha wananchi wanapata makazi bora.
“Tatizo la makazi duni kwa wananchi husababisha afya mbovu na hivyo kupunguza nguvu ya uzalishaji je serikali ina mkakati gani kuhakikisha wananchi wanapata makazi bora,” alihoji Peneza.
Akijibu maswali hayo Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Angella Mabura amesema suala la kupunguza kodi ya vifaa vya ujenzi linatakiwa kupitiwa upya ili kuondokana na mkanganyiko ambao unaweza kujitokeza.
Amesema suala hilo la kupunguza kodi ya vifaa vya ujenzi lilijadiliwa lakini ilionekana kuwepo katika mkanganyiko kutokana na kuwepo kwa punguzo katika shirika la nyumba.
Kuhusu sheria ya madini, Mabura amesema sheria hiyo ipo vizuri lakini imekuwa ikitekelezwa vibaya kwa wanaoisimamia na serikali itahakikisha inasimamia haki na sheria hiyo.
Mbali na hilo Mabura amesema serikali inatoa rai kwa mamlaka za serikali za mitaa kutenga fedha za kutosha katika bajeti zao kila mwaka kwa ajili ya kuongeza kiasi cha kupima, kupanga na kumilikisha ardhi katika maeneo yao ili kuwawezesha wananchi kupata makazi bora.
Leave a comment