BARAZA la Vijana la Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Bavicha), limeishauri Kamati Kuu ya Chadema kuwafukuza uanachama, wanachama 19 waliokwenda kinyume na msimamo wa chama hicho, kwa kukubali uteuzi wa ubunge viti maalumu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Hayo amesema Mwenyekiti wa Bavicha, John Pambalu leo Alhamisi tarehe 26 Novemba 2020, wakati anazungumza na waandishi wa habari makao makuu ya Chadema, Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Pambalu alikuwa akitoa msimamo wa baraza hilo, baada ya kamati tendaji kukutana katika mkutano jana usiku Jumatano kwa njia ya mtandao kujadili wanachama hao 19 waliokwenda kuapishwa kuwa wabunge wa viti maalum.
Wanachama hao 19 wakiongozwa na Mwemyekiti wa Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha), Halima Mdee, waliapishwa kuwa wabunge viti maalumu na Spika Job Ndugai, tarehe 24 Novemba 2020, kwenye viwanja vya Bunge jijini Dodoma.
Akitangaza maazimio ya kamati tendaji hiyo ya Bavicha, Pambalu amesema, baraza hilo linaishauri kamati kuu hiyo ya Chadema kuwachukulia hatua kali za kinidhamu wabunge hao viti maalumu.
Mwenyekiti huyo amesema, miongoni mwa hatua kali hizo, ni kuwafukuza uanachama.

“Ziko adhabu nyingi za kuchukuliwa kwa hao 19, kuvuliwa nyadhifa zao, kunyang’anywa uanachama wao. Dhambi ya usaliti ni dhambi mbaya. Hatutaki kushinikiza Kamati Kuu ichukue hatua gani. Lakini hatua kali zichukuliwe ikiwemo kuwafukuza uanachama wao, “amesema Pambalu.
Pambalu amesema, wanachama hao wamekisaliti chama hicho, hivyo wanapaswa kwenda katika vyama ambavyo usaliti ni kosa la kawaida.
“Lakini siku zote wasaliti ndani ya Chadema si mahala salama kwa wao, wanaweza kuchagua kwenda katika chama ambacho usaliti ni kawaida. Chama chetu usaliti si kosa la kawaida,” amesema Pambalu.
Pambalu amesema, maazimio hayo yalitolewa usiku wa jana tarehe 25 Novemba 2020, katika cha dharula cha Kamati Tendaji ya Bavicha.

“Kilichofanywa ni kitendo cha usaliti na hujuma hakiwezi kivumilika na taasisi yoyote kwa kuwa katibu mkuu (John Mnyika) anasema wanaruhusu maoni ili chama kichukue hatua. Sisi kamati tendaji ya Bavicha, tunaishauri kamati kuu ya chama ichukue hatua kali ya kinidhamu kwa ajili ya mustakabali wa chama,” amesema Pambalu.
Wabunge wengine walioapishwa ni wajumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Ester Bulaya na Esther Matiko. Katibu Mkuu wa Bavicha, Nusrat Hanje. Katibu Mkuu Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha), na Grace Tendega.
Makamu Mwenyekiti Bawacha, Hawa Mwaifunga. Naibu Katibu Mkuu Bawacha, Jesca Kishoa na Katibu Mwenezi Bawacha, Agnesta Lambat.
Mwenyekiti wa Chadema Mkoa Mtwara, Tunza Malapo. Ceciia Pareso. Asia Mwadin Mohamed. Felister Njau. Naghenjwa Kaboyoka. Sophia Mwakagenda. Kunti Majala. Stella Siyao.Salome Makamba. Anatropia Theonest na Conchesta Lwamlaza.
Kuhusu Katibu Mkuu wa Bavicha, Nusrat Hanje ambaye ni miongoni mwa hao 19, Pambalu amesema, baraza hilo limeshindwa kumchukulia hatua kwa kuwa hakuitikia wito wa Kamati Tendaji kwa ajili ya kujieleza.
“Kwa kuwa juhudi za kumtafuta Nusrat Hanje ajieleze mbele ya kamati tendaji yetu hazikuzaa matunda, hakuweza kwa kuwa kupatikana. Tumeshindwa kuchukua hatua, tunaiachia Kamati Kuu ya Chadema,” amesema Pambalu.
Pambalu amesema, Bavicha linaichia Kamati Kuu ya Chadema jukumu la kumuadhibu Hanje.
“Laiti tungempata na kumsikilzia kwa ajili ya kuhehsimu nidhamu, tungeweza kutoka na mazimio yetu kama Bavicha, kwa kuwa tungepata fusa ya kumsikiliza. Lakini kwa kuwa ataitwa tunaiachia kamati kuu ya chama ambayo mimi ni mjumbe nitapeleka mapendekezo nini vijana wanashauri ichukue hatua dhidi yake,” amesema Pambalu.
Licha ya msimamo huo wa Bavicha, Chadema kimewaita wanachama wake 19 walioapishwa kuwa wabunge viti maalumu wajieleze kwa nini wamekiuka maagizo ya chama hicho kwa kukubali uteuzi huo.
Wabunge hao wanatakiwa kuitikia wito huo kesho Ijumaa tarehe 27 Novemba 2020 saa 2:00 asubuhi makao makuu ya Chadema, Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Chadema kikishirikiana na Chama cha ACT-Wazalendo, vimegoma kupeleka wawakilishi wake bungeni na katika Baraza la Wawakilishi la Zanzibar, wakipinga matokeo ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika tarehe 28 Oktoba 2020 kwa madai kwamba mchakato wake haukuwa huru na wa haki.
Matokeo hayo yaliyotangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi Tanzania (NEC), yalikipa ushindi wa kishindo Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika nafasi za urais wa Tanzania na Zanzibar, ubunge, uwakilishi na udiwani.
Huku vyama vya upinzani, Chadema na Chama cha Wananchi (CUF) vikiambulia jimbo moja kwa kila chama upande wa Bara. Huku ACT-Wazalendo kikiambulia majimbo manne upande wa Zanzibar.
johnmandera218@gmail.com.