MWANASIASA mkongwe nchini Tanzania, Basil Pesambili Mramba (81) , amefariki dunia katika Hospitali ya Regency, jijini Dar es Salaam, alikokuwa anapatiwa matibabu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa ya kifo hicho imetolewa na ndugu wa marehemu, Godfrey Mramba.
Godfrey amesema Mramba Mramba amefariki dunia leo Jumanne, tarehe 17 Agosti 2021, alipokuwa anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Regency.
Mramba amesema, amezaliwa tarehe 15 Mei, 1940, kuondoka tarehe 17 Agosti 2021.
“Kwa masikitiko familia ya Mramba inatangaza kifo cha baba yetu mpendwa, Basil Pesambili Mramba,” imeeleza taarifa ya Godfrey.
Godfrey amesema, kutokana na janga la Ugonjwa wa Korona (UVIKO-19), familia itafanya mazishi binafsi.
“Kwa kuzingatia hali ya janga, familia inapokea sala zenu na tunaomba faragha. Tutapokea wageni kutoka kwenye familia pekee katika makazi yake yaliyopo Mawenzi Road Oysterbay,” amesema Godfrey.
Godfrey amesema msiba huo uko nyumbani kwa marehemu Mramba, Oysterbay jijini Dar es Salaam na kwamba ratiba ya mazishi itatolewa baadae.
Enzi za uhai wake, aliwahi kuwa Waziri wa Fedha (2001 hadi Desemba 2005). Waziri wa Viwanda na Biashara (2006 hadi 2008).
Pia, alikuwa Mbunge wa Rombo mkoani Kilimanjaro, kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Kutokana na utumishi wake, Mramba na Daniel Yona aliyekuwa waziri wa Nishati na Madini mwaka 2016, walihukumiwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kwenda jela miaka mitatu kwa matumizi mabaya ya madaraka kuisababishia serikali hasara ya shilingi bilioni 11.7
Hata hivyo, baada ya kutumikia adhabu hiyo kwa mwaka mmoja, walipunguziwa na kufungwa kifungo cha nje kuanzia Februari hadi tarehe 9 Novemba mwaka 2016, wakitakiwa kufanya kazi za jamii.
Mungu ailaze roho ya Marehemu mahala pema poponi