WAZIRI wa Kilimo, Hussein Bashe, amemuomba Rais Samia Suluhu Hassan, atoe Sh 150 bilioni, kwa ajili ya kutoa ruzuku kwa wakulima kwa ajili ya kumudu gharama za mbolea. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Bashe ametoa ombi hilo leo Jumatatu, tarehe 4 Aprili 2022, katika uzinduzi wa ugawaji vitendea kazi kwa maafisa ugani uliofanyika jijini Dodoma, ambapo Rais Samia ni mgeni rasmi.
Waziri huyo wa kilimo, amesema kwa sasa dunia inakabiliwa na mfumuko wa bei ya mbolea, ambayo bei yake imepanda kwa asilimia 300.
“Nataka nikuombe Rais kwa kuwa uliwaagiza Benki Kuu watenge Sh. 1 trilioni kwa ajili ya sekta ya kilimo, nakuomba Sh. 150 bilioni tuiweke kwenye benki tuanze kutoa ruzuku ya mbolea kwa kuanzia msimu ujao wa kilimo. Nikuhakikishie pesa hii haitapotea,” amesema Bashe.
Aidha, Bashe amesema wizara yake itaendelea kutatua changamoto za wakulima hasa wanaolima malighafi za kutengenezea mafuta, ili kuongeza uzalishaji kwa ajili ya kukabiliana na uhaba wa mafuta ya kula nchini.
“Tuna changamoto ya mafuta ya kula, umetoa maelekezo kwamba tuhakikishe tunalitatua tatizo la mafuta. Katika nchi yetu mahitaji yake ni tani 650,000, uzalishaji wa ndani hauzidi 250,000, tuna pengo la 400,000. Ili kukabiliana na upungufu, Wizara tumetoa miche zaidi ya 1,500,000 ya michikichi,” amesema Bashe.
Bashe amesema, msimu ujao wa kilimo, wizara yake itazalisha tani 5,000 za mbegu ya alizeti, ili kuongeza uzalishaji wa zao hilo kwa ajili ya kuoata rasilimali za kutosha za kutengenezea mafuta ya kula.
Katika hatua nyingine, Bashe ameiomba Serikali kupunguza kodi kwa bidhaa za mafuta zinazoingizwa nchini pamoja na zile zinazozalishwa na viwanda vya ndani.
Bashe amesema wizara ya kilimo imeweka mikakati ya kupandisha mapato yatokanayo katika sekta ya kilimo, kutoka asilimia tano iliyoko sasa, hadi asilimia 10 ifikapo 2030.
Leave a comment