KLABU ya Barcelona imemuachia nyota wake Neymar kuondoka katika timu hiyo na kujiunga na Paris St. German (PSG) kwa kitita cha pauni 198 milioni, anaandika Hamisi Mguta.
Neymar ambaye ni raia wa Brazil amepewa ruhusa na meneja Ernesto Valvarde asifanye mazoezi na badala yake kushughulikia mpango wa uhamisho wake na amewaambia wachezaji wenzake wakati wa mazoezi siku ya leo Jumatano kwamba angependa kuondoka.
Mshambuliaji huyo ataruhusiwa kuondoka kwa gharama ya Euro milioni 222, ambazo PSG iko tayari kulipa.
Hatua hiyo ni siku mbili baada ya kubainika kwamba Barcelona ilikuwa tayari kuruhusu uchunguzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani (Fifa) iwapo PSG ingemsajili Neymar.
Rais wa La Liga Javier Tebas alitishia kuchukua hatua za kisheria dhidi ya mabingwa hao wa zamani wa Ligi 1 iwapo soka ya Ulaya itashindwa kuchukua hatua.
Pia alisema kuwa rais wa PSG, Nasser Al Khelafi alijulishwa kuhusu malengo ya mabingwa hao wa Uhispania.
Neymar alihamia Barcelona kutoka klabu ya Santos nchini Brazil 2013 kwa uhamisho wa pauni 46.6 milioni na kusaini mkataba wa miaka mitano na mabingwa hao wa Uhispania 2016.
Leave a comment