SERIKALI imepanga kufanya usanifu na thathmini ya gharama za ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami katika Mji wa Ikungi. Anaripoti Jemima Samwel, DMC … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 21 Aprili 2021, bungeni jijini Dodoma na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi).
Ni baada ya Miraji Jumanne, Mbunge wa Singida Mashariki kuiomba serikali ielezee, lini itatekeleza ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami wilayani Ikungi.
“Katika mwaka wa fedha 2021/22, serikali kupita wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), imepanga kufanya usanifu wa tathmini ya gharama za ujenzi wa barabara zenye umuhimu kwa kiwango cha lami katika Mji wa Ikungi.
“Hadi Machi 2021, TARURA imetoa Sh. 598.22 Milioni kati ya Sh. 890.89 Milioni zilizotengwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilometa 97.92 katika Wilaya ya Ikungi,” taarifa ya Tamisemi imeeleza.
Na kwamba, katika mwaka wa fedha 2021/22, serikali itaomba kuidhinisha Sh. 925.08 Milioni kwa ajili ya matengenezo ya barabara zenye urefu wa 92.6 kilomita, vilevile Sh. 1.4 Bilioni zitatengwa kwa ajili ya ujenzi wa Daraja la Mihyuge, Wilaya ya Ikungi.
“Serikali itaendelea kufanya usanifu wa kujenga barabara kwa kiwango cha lami kwenye maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Ikungi kulingana na upatikanaji wa fedha,” imeeleza Tamisemi.
Leave a comment