SERIKALI ya Tanzania imetenga jumla ya Sh. 5.96 Bilioni, kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara ya Kibena –Lupembe, mkoani Njombe. Anaripoti Nasra Bakari, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumanne tarehe 20 Aprili 2021, na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, Dk. Leonard Chamurilo, wakati inajibu swali la Mbunge wa Lupembe, Edwin Enosy Swale, bungeni jijini Dodoma.
Katika swali lake, Swale alihoji lini ujenzi wa barabara ya Kibena hadi Madeke yenye urefu wa kilimomita 125, utaanza kujengwa kwa kiwango cha lami.
Ikijibu swali hilo, Wizara ya Ujenzi imesema Serikali kwa mwaka wa fedha wa 2020/21, imetenga kiasi hicho cha fedha, kwa ajili kuanza kujenga kipande cha barabara hiyo chenye urefu wa kilomita 50, kwa kiwango cha lami.
“Katika mwaka wa fedha 2021, Serikali imetenga jumla ya Sh. 5.96 Bil. kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami wa sehemu ya barabara ya Kibena – Lupembe (km 50),” imesema Wazara ya Ujenzi.
Hata hivyo, Wizara ya Ujenzi imesema, itaendelea kuhudumia barabara hiyo ili ipitike katika majira yote, wakati inatafuta fedha za kumalizia kuijenga kwa kiwango cha lami.
“Aidha, wakati Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami kwa vipande vingine. Wizara yangu inaendelea kuihudumia barabara hiyo ili iweze kupitika majira yote ya mwaka,” imesema Wizara huyo.
Leave a comment