MWENYEKITI wa Chama cha Ukombozi wa Umma (Chaumma), Hashim Rungwe, amestaajabishwa na hatua ya Spika wa Bunge, Job Ndugai, kushangilia Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha wa 2021/22, ya Sh. 36.3 trilioni, kupitishwa bila kupingwa bungeni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Bajeti hiyo ilipitishwa jana tarehe 23 Juni 2021, bungeni jijini Dodoma, kwa kura za ndiyo 361 (94%), kati ya 385 za wabunge walioshiriki zoezi hilo, huku 23 (6%) zikiwa ni kura zisizokuwa na upande ‘Abstain’. Kura za hapana hazikuwepo.
Akizungumza na MwanaHALISI Online leo tarehe 23 Juni 2021, ofisini kwake Makumbusho jijini Dar es Salaam, Rungwe amesema, Spika Ndugai hakupaswa kushangilia kitendo hicho, kwa kuwa kilitarajiwa kufanyika, kwani Bunge hilo lina asilimia kubwa ya wabunge wa Chama tawala Cha Mapinduzi (CCM).
“Spika mwenyewe ndiyo unamuona hivyo, yeye yuko pale anasifia mimi sijawahi kuona. Wewe hujawahi kuona wakati unajua wabunge wote wa CCM, we hujawahi kuona kitu gani? Ungeshangaa kama wabunge asilimia kubwa sio wa CCM na wote wamepiga kura, lakini vinginevyo ni mtu anayestajaabisha,” amesema Rungwe.
Kura za ndio 361 zilipigwa na wabunge wa CCM, huku zisizokuwa na upande zikipigwa na wabunge wa upinzani 24, ambapo 19 ni wa viti maalumu waliovuliwa uanachama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo Novemba 2020, wanne ni wa ACT-Wazalendo na mmoja wa Chama cha Wananchi (CUF).
Akizungumzia bajeti hiyo, Rungwe amesema ni mapema mno kuichambua kwa kuwa utekelezaji wake bado.
“Ile ni bajeti tu bado utekelezaji wake, bajeti hii very cosmetic (imepambwa), imepambwa sana utafikiri mwali vile anapendeza. Lakini tunangoja kuona vitendo vyake, maana huwezi kuirudisha nyuma, si unaona wenyewe wanapiga makofi wote wanaikubali na lazima waikubali,” amesema Rungwe.
Baada ya wabunge kuipitisha bajeti hiyo, Spika Ndugai alisema haijawahi kutokea bajeti kupitishwa bila ya kupigiwa kura ya hapana.
“Kura za hapana kwa mara ya kwanza hakuna hata moja, kura za ambao hawakuamua ni 23, yaani walio-Abstain ni 23. Waliokubali kupitisha bajeti hii ni 361 ambayo ni asilimia 94, asilimia hii ni kubwa kabisa ambayo katika kumbukumbu za Bunge miaka ya karibuni haijapata kutokea,” alisema Spika Ndugai.
Leave a comment