WAKATI mwaka mmoja wa kukamilisha bajeti yake, ukifikia ukingoni, Serikali ya awamu ya sita imelenga kuongeza zaidi ukuaji uchumi kwa mwaka wa fedha 2022/23. Anaripoti Mwandishi Wetu Dodoma … (endelea)
Kwa mujibu wa taarifa ya mapendekezo ya ukomo wa bajeti kwa mwaka 2022/23 Serikali imelenga kukusanya na kutumia Sh. 41 Trilioni.
Bajeti hiyo ni sawa na ongezeko la asilimia 8 la bajeti ya mwaka 2021/22 ya Sh. 37.9 Trilioni na imekuja na shabaha na malengo ya uchumi jumla kwa mwaka ujao wa fedha.
Hadi sasa ukuaji wa Pato la Taifa kufikia Desemba 2021 ni asilimia 4.9 sawa na ongezeko la asilimia 0.1 kutoka ukuaji wa asilimia 4.8 mwaka 2020.
Hata hivyo Serikali ya awamu ya sita imelenga kufikia ukuaji wa pato la taifa wa asilimia 5.2 mwaka 2022 kutoka matarajio ya ukuaji wa asilimia 5.0 mwaka 2021.
Pia imelenga kuendelea kudhibiti kasi ya mfumuko wa bei na kuhakikisha kuwa unabaki kwenye wigo wa tarakimu moja ya wastani wa asilimia kati ya 3.0 – 5.0 katika muda wa kati.
Vilevile imelenga mapato ya ndani (ikijumuisha mapato ya Halmashauri), kufikia asilimia 16.3 ya Pato la Taifa mwaka 2022/23 huku mapato ya kodi kufikia asilimia 13.8 ya Pato la Taifa mwaka 2022/23 kutoka matarajio ya asilimia 13.3 mwaka 2021/22.
Aidha imelenga kuhakikisha kuwa nakisi ya bajeti haizidi asilimia 3.0 ya Pato la Taifa na kuwa na akiba ya fedha za kigeni kwa kiwango cha kukidhi mahitaji ya uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje kwa kipindi kisichopungua miezi minne (4).
Leave a comment