ASILIMIA 94 ya Wabunge wa Bunge la Jamhuri Tanzania, jijini Dodoma wamepitisha Bajeti Kuu ya serikali ya Sh. 36.3 Trilioni kwa mwaka wa fedha 2021/2022. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Bajeti hiyo imepitishwa leo Jumanne, tarehe 22 Juni 2021, baaada ya wabunge kupiga kura ya wazi, kufuatia kufungwa mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali, kwa mwaka huo wa fedha.
Akitoa matokeo ya zoezi hilo, Spika Job Ndugai amesema, wabunge 23 kati ya 385 waliohudhuria bungeni, wamepiga kura ya wasiokuwa na upande (Abstain) huku 361 wakipiga kura ya ndiyo.
Bunge la Tanzania
“Kura za hapana kwa mara ya kwanza hakuna hata moja, kura za ambao hawakuamua ni 23, yaani walio-Abstain ni 23. Idadi ya wabunge wote waliokuwemo humu bungeni ilikuwa 385, wabunge waliokuwa hawapo watano, hivyo ambao hawakuamua ni asilimia 6,” amesema Spika Ndugai.
Spika Ndugai ameongeza “na waliokubali kupitisha bajeti hii ni 361 ambayo ni asilimia 94, asilimia hii ni kubwa kabisa ambayo katika kumbukumbu za bunge miaka ya karibuni haijapata kutokea.”
Bajeti hiyo imepitishwa baada ya wabunge kuijadili kwa muda wa siku sita, tangu ilipowasilishwa bungeni na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba, tarehe 10 Juni mwaka huu.
Leave a comment