SHAUKU ya Watanzania kuwashuhudia mabondi wenye viwango vya juu kwa sasa nchini humo, Twaha Rubaha maarufu ‘Twaha Kiduku’ na Hassan Mwakinyo wakipanda ulingo, linaweza kufikiwa baada ya Gari jipya aina ya V8 ya mwaka 2020 kuwekwa mezani ili “wazichape.” Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Gari hilo linalofikia thamani ya zaidi ya Sh.200 milioni, likiwa limelipiwa kodi, limetangazwa kutolewa na Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki (CCM), Hamis Taletale maarufu Babu Tale.
Babu Tale ametangaza kutoa gari hilo baada ya Twaha Kiduku anayetokea Morogoro kuibuka mshindi dhidi ya Abdallah Pazi maarufu Dulla Mbabe kwenye pambano lililopewa jina la ‘Payback.’
Pambano hilo la raundi 10, lililofanyika jijini Dar es Salaam usiku wa kuamkia leo Jumamosi tarehe 21 Agosti 2021 lilishuhudia Twaha Kiduku akimpiga kwa pointi mshindani wake Dulla Mbabe.
Katika pambano hilo, lilishuhudiwa Kiduku akidondoshwa raundi ya kwanza baada ya kupigwa konde na Dulla Mbabe ambalo alishindwa kuhimili na baada ya kurejea raundi zingine, Dulla alipelekewa masumbwi mfululizo.
Ushindi huo, ulimfanya Twaha Kiduku kuwa mbabe wa Dulla baada ya kumpiga mara mbili katika mapambano matatu waliyokwisha kucheza huku moja walitoka sare.
Twaha Kiduku ameondoka na gari jipya aina ya Crown.
Baada ya ushindi huo, Babu Tale ambaye pia ni meneja wa msanii maarufu nchini Tanzania, Diamond Platinum amemweleza mbunge wenzake wa CCM jimbo la Muhenza mkoani Tanga, Hamis Mwinjuma maarufu ‘Mwana FA’ amshauri Hassan Mwakinyo akubali pambano na Twaha Kiduku.
Babu Tale ni mbunge wa kutoka Mkoa wa Morogoro anakoishi Twaha Kiduku na Mwana FA ni wa Tanga ambako anatoka Hassan Mwakinyo.
“Wapeni salaam Morogoro ndio mkoa pekee unaobeba magari yenu yooote ya Dar.. Tanga eeeh kubalini basi tumalize hili jambo,naweka V8 ya mwaka 2020… Oya @mwanafa mjuze mwanao basi. Asante @twaha_kidukuumetuheshimisha wana Morogoro,” ameandika Babu Tale.
Asanteni sana kwa taarifa,
Hebu tusubiri kama kweli hiyo V8 itaenda Morogoro.
Rafiki yenu,
Aliko Musa.
Mbobezi Kwenye Majengo