UAMUZI wa Zitto Kabwe, Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo kugombea tena Jimbo la Kigoma Mjini, umenisukuma kugombea tena Kata ya Mwanga Kaskazini. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam…(endelea).
Ni kauli ya Msanii wa Muziki wa Kizazi Kipya (Bongo Fleva) na aliyekuwa Diwani wa Kata ya Mwanga Kaskazini (ACT-Wazalendo), Clayton Revocatus maarufu Baba Levo aliyoitoa leo
tarehe 22 Julai 2020, katika mkutano wake na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
“Mara ya kwanza niliwaita waandishi wa habari na nikawaambia, nimetia nia kugombea ubunge Kigoma Mjini kama Zitto hatogombea jimbo hilo.
“Lengo langu kubwa lilikuwa ni kuzuia ‘virusi’ cha wasio na uwezo wa kuwaongoza wananchi au kupata ubunge, halafu wana kieherehere cha kutaka kugombea,” amesema Baba Levo.
Pia Baba Levo amesifu wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa kuwatosa waigizaji na wachekeshaji kwenye kura za maoni ya chama hicho.
“Wengi ni viherehere, walienda kama nyumbu lakini mwisho wa siku wamekuja kuwa wa mwisho, wengine wamekosa kura kabisa kwenye mchakato wa kura za maoni,” amesema.
Amesema, baada ya watu kusikia Zitto hatorudi kugombea Jimbo la Kigoma Mjini, ilionekana jimbo lingekuwa jepesi kwa mtu yeyote kushinda.
“Nimefurahishwa sana na wale waliopuuzwa ingawa nimesikia kwamba mchakato bado unaendelea na wanaweza kurudishwa, lakini natamani iendelee hivyo ili viherehere wakae pembeni.
“Naomba kutangaza wazi kwamba, tayari nimeshajaza fomu na nimesharudisha kimyaa kimyaa. Tunasubiri filimbi ilie,” amesema.
Leave a comment