TAIFA la Somalia liko mbioni kuwa mwanachama rasmi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), baada ya timu iliyoundwa na taasisi hiyo kutathmini maombi yake kuhitimisha majukumu yake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana tarehe 3 Februari 2023 na EAC kupitia ukurasa wake wa Twitter, timu hiyo ilihitimisha zoezi lake la kutathimini utayari wa Somalia kujiunga na jumuiyo, kwa kufanya majadiliano na Jaji Mkuu wake, Bashe Yusuf Ahmed, mjini Mogadishu.
Taarifa hiyo imesema kuwa, ripoti ya uhakiki ya timu hiyo inatarajiwa kuwasilishwa katika Baraza la Mawaziri wa EAC, ambao wataiwasilisha kwenye mkutano wa 23 wa wakuu wa nchi unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa Februari mwaka huu.
“Timu ya uhakiki ya EAC inayotathmini utayari wa Somalia kujiunga na jumuiya ilihitimisha ujumbe huo kwa kufanya mazungumzo na Jaji Ahmed. Ripoti ya uhakiki inatazamiwa kuwasilishwa katika Baraza la Mawaziri wa EAC ambao wataiwasilisha kwa ajili ya kupitiwa kwenye mkutano wa 23 wa wakuu wa nchi unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa Februari,” imeeleza taarifa hiyo.
Oktoba 2022 Rais wa Somalia, Hassan Sheikh Mohamud, alitoa wito wa nchi yake kukubaliwa kujiunga na EAC akisema kwamba ni sehemu ya ukanda wa Afrika Mashariki lakini pia ni ndoto ya wananchi wake.
Rais Mohamud alisema kuwa, hakuna nchi ya Jumuiya hiyo ambayo haifanyi biashara na Somalia, lakini pia tamaduni za nchi yake zinafanana na nchi za ukanda huo.
Kufuatia ombi hilo, EAC mnamo Januari 2023, ilizindua rasmi ujumbe wa kutathimini na kuthibitisha utayari wa Somalia kujiunga na jumuiya hiyo.
Somalia imewasilisha ombi hilo baada ya wakuu wa nchi wa jumuiya hiyo mnamo Machi 2022, kuipitisha rasmi nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (Congo DR), kuwa mwanachama wa EAC, ambapo imekuwa mwanachama wa saba.
Miongoni mwa nchi nyingine wanachama wa EAC ni Tanzania, Uganda, Kenya, Rwanda na Burundi.
Hata hivyo, baadhi ya watu walionyesha wasiwasi wao kuhusu Somalia kujiunga na jumuiya hiyo kutokana na changamoto za kiusalama inazopitia.
Leave a comment