BUNGE la Tanzania litapitisha azimio la kuibana Serikali ya nchi hiyo kutobadili uamuzi wa kuhamisha shughuli za Serikali kutoka jijini Dodoma kwenda kwingine. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea)
Bunge hilo linaloongozwa na Spika Job Ndugai, lilikwisha kupitisha sheria ya kuifanya Dodoma kuwa makao makuu ya nchi.
Orodha za shughuli za Bunge za leo Jumatatu tarehe 8 Juni 2020 zilizotolewa na Katibu wa Bunge, Stephen Kagaigai zinaonyesha, miongoni mwa shughuli ni kupitisha “Azimio la Bunge la kuitaka Serikali kutobadili uamuzi wa Jiji la Dodoma kuwa Makao Makuu ya nchi na shughuli za Serikali;.”
Azimio hilo litapitishwa kipindi ambacho tayari shughuli nyingi za Serikali zimehamia Dodoma kutoka Dar es Salaam ikiwemo, Rais wa nchi hiyo, John Pombe Magufuli.
Wizara zote, Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa nao wamehamia Dodoma.
Uamuzi wa kuhamishia shughuli za Serikali Dodoma, ilikuwa miongoni mwa ahadi za Rais Magufuli katika kampeni zake kuwa katika kipindi chake cha miaka mitano kati ya 2015na 2020 atahakikisha anahamia Dodoma.
Tarehe 30 Mei 2020, Rais Magufuli aliwaongoza marais wastaafu uwekaji wa kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Ikulu eneo la Chamwino nje kidogo ya Jiji Dodoma.
Hafla hiyo ilihudhuliwa na Mama Maria Nyerere kwa niaba ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere na marais wastaafu, Ali Hassani Mwinyi, Benjamini Mkapa na Jakaya Kikwete.
Akizungumza katika hafla hiyo, Rais Magufuli alisema wakati wa kampeni 2015 aliahidi ndani ya miaka mitano ya utawala wake, serikali yote itakuwa imehamia Dodoma kama ilivyokuwa ndoto ya Mwalimu Nyerere.
“Niliahidi ndani ya miaka miatano Serikali yote itahamia Dodoma, lakini sikuwa na uhakika kama nitafanikisha, lakini namshukuru Mungu imewezekana, watumishi na wizara zote zimehamia Dodoma,” alisema Rais Magufuli.
Leave a comment