MATAJIRI wa jiji la Dar es Salaam – Azam FC leo tarehe 29 Agosti, 2022 wamethibitisha kumbadilishia majukumu kocha wao mkuu, Abdihamid Maollin na Msaidizi wake, Omary Nasser kutokana na kile kilichodaiwa kuwa mwenendo usioridhisha wa timu hiyo. Anaripoti Damas Ndelema, Dar es Salaam … (endelea).
Kupitia taarifa iliyotolewa na ukurasa wa Instagram wa timu hiyo imeeleza kuwa wamefikia makubaliano baina ya pande zote mbili kati ya uongozi wa timu na makocha hao amabapo wataachia ngazi kama kocha mkuu na kocha msaidizi lakini wataendelea kubaki kuwa sehemu ya klabu hiyo.
Wawili hao wanatarajiwa kupewa majukumu mengine tofauti katika idara ya ufundi ambapo nafasi hizo zitatangazwa hapo badae
Kocha huyo alijiunga na Azam msimu uliopita wa 2021/22 akichukua mikoba ya George Lwandamina na kuisaidia Azam kufika fainali ya kombe la mapinduzi na kupoteza dhidi ya Simba.
Pia walifanikiwa kufika nusu fainali ya kombe la Shirikisho la Azam na kutolewa na Coastal Union na kufanikiwa kushika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi kuu ya NBC.
Aidha, klabu hiyo itakuwa chini ya kocha wa makipa Daniel Cadena ambae ni kocha wa makipa mwenye leseni ya juu kabisa ya ukocha UEFA Pro Licesence hivyo ataiongoza timu hiyo mpaka pale uongozi utakapomtangaza kocha mpya.
Mpaka sasa msimu huu kwenye Ligi kuu ya NBC, Azam wamecheza mechi mbili na kushinda mechi moja dhidi ya Kagera Sugar na kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Geita Gold.
Wenyeji hao wa Chamanzi wanatarajiwa kurejea tena uwanjani tarehe 6 Septemba mwaka huu dhidi ya Yanga katika uwanja wa Benjamini Mkapa.
Leave a comment