Asasi mbalimbali za kiraia – AZAKI zimeibana Serikali na kuitaka ieleze ni faida iliyopatikana tangu yalipofanyika kwa Marekebisho ya Sheria ya Madini ya mwaka 2017. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Pia zimeiomba Serikali kueleza iwapo mfumo wa sasa wa maamuzi ya fedha kwenye sekta ya madini unatosha kuipatia nchi faida na wawekezaji ili kuendeleza ushindani.
Maswali hayo yameibuliwa jana tarehe 25 Oktoba mwaka huu jijini Dodoma na Mkurugenzi Mtendaji wa Hakirasilimali, Rachel Chagonja katika mdahalo kuhusu faida ya madini nchini.
Chagonja alielekeza maswali hayo kwa Waziri wa Madini, Dotto Biteko wakati alipokaribishwa kwenye majadiliano yaliyoandaliwa na Azaki ikiwa ni Maadhimisho ya Wiki ya Azaki yaliyofanyika kitaifa Jijini Dodoma yakiwa na kaulimbiu ya ‘Mchango wa Azaki kwa Maendeleo ya Nchi’.
Akijibu maswali hayo Waziri wa Madini, Dotto Biteko amesema pamoja na jitihada kubwa za mabadiliko ya sheria ya madini ya mwaka 2017, bado sekta hiyo inachangamoto ndogondogo ambazo bado zinaendelea kufanyiwa kazi.
Hata hivyo, amesema tangu Tanzania ipate Uhuru sekta ya madini ilikuwa haijawai kufanya vizuri kutokana na uwepo wa sheria ambazo zilikuwa zimetokana na sheria za kikoloni.
“Tanzania baada ya kupata Uhuru tulikuwa na kiu kubwa ya kusimamia rasilimali zetu wenyewe ndiyo maana hata baba wa Taifa Kambarage Nyerere hakutaka kuzichimba kwa kuwa bado hatukuwa na uwezo.
“Hata hivyo, watu wengi walilalamika kwa madai kuwa wanakosa manufaa kutoka sekta ya madini na waka 2002 kamati nyingi ziliundwa Bungeni na serikali ambapo kamati ya mwisho ilikuwa ya Jaji Bomani” alieleza Dotto.
Alisema sheria hiyo ililenga kubadilisha uchumi wa taifa na wa eneo husika mathalani kama mgodi upo Dodoma na eneo la mkoa huo libadilike na kukua kiuchumi.
Akizungumzia kuazishwa kwa sheria ya Madini ya mwaka 2017, Biteko amesema ilifanyiwa marekebisho ili kupata uhalali wa kujadili mikataba iliyokuwa ikilalamikiwa.
Akizungumzia faida za marekebisho hayo amesema imewapa manufaa makubwa kwa wachimbaji wadogo ambao kwani hapo awali walikuwa wananyanyasiwa kwa namna mbalimbali
Aidha, Biteko amesema mwaka jana matarajio ya Serikali ilikuwa kukusanya Sh. bilioni 526 lakini kabla ya mwaka wa fedha sekta ya madini ilikuwa imekusanya Sh. bilioni 586 na kuifanya sekta hiyo kwa mara ya kwanza kuongoza ikifuatiwa sekta ya ujenzi.
Amesema katika kuonesha mafanikio sekta ya madini imefungua migodi mingi mipya mipya ambayo haijawahi kuanzishwa.
Leave a comment