ASKOFU Emmaus Mwamakula, Mkuu wa Kanisa la Moravian la Uamsho Tanzania, ameiomba Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) nchini Tanzania, kuwarudisha wagombea wa vyama vya upinzani walioenguliwa na wasimamizi wa uchaguzi kinyume na sheria. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Askofu Mwamakula ametoa wito huo leo Jumatatu tarehe 31 Agosti 2020, katika uzinduzi wa Ilani ya Uchaguzi Mkuu wa 2020 ya Chama cha ACT-Wazalendo uliofanyika katika Hoteli ya Protea jijini Dar es Salaam.
Kiongozi huyo wa koroho amesema, wagombea hao walioenguliwa wakirudishwa, Uchaguzi Mkuu wa Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020 hautakuwa wa malalamiko bali utakuwa wa huru na haki.
“Nitoe wito kwa NEC, hao watu wako chini yao maana wao wako chini watatafuta taratibu zao, lakini wahakikishe wagombea walioenguliwa katika ngazi zote, warudishwe mkifanya hivyo itakuwa dalili njema, tutakuwa na uchaguzi wa huru na haki. Kama wanaenguliwa hivi, je wakati wa kutangazwa itakuwaje?” amehoji Askofu Mwamakula.
Askofu Mwamakula amesisitiza, baadhi ya wagombea walioenguliwa kinyume na sheria warudishwe bila masharti yoyote.
“Nilipokuwa Chadema nazindua kampeni na nitaendelea kusema kwamba katika hili, niwatake wasimamisi wasaidizi wa wanaohusika ngazi za jimbo, kata na Zanzibar kama kuna rufaa zipo mezani kwao wanayo nafasi ya kutengeneza sasa,
Kama kuna jambo linalalamikiwa wanayo nafasi ya kutengeneza sasa wawarudishe watu pasipo masharti yoyote ” amesema Askofu Mwamakula.
Chama cha ACT-Wasalendo kimemsimamisha Bernard Membe ambaye ni mwanachama wake mpya kugombea urais wa Tanzania, mgombea mwenza wake ni Prof. Omary Fakhi Hamad.
Membe alikuwa mwanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambaye alifukuzwa kwa madai ya kwenda kinyume na taratibu za chama hicho.
Leave a comment