ASKOFU Mkuu Yuda Thaddeus Ruwa’ichi, wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, amesema uchunguzi dhidi ya chanzo cha kifo cha aliyekuwa Mkuu wa Wamisionari Afrika nchini Tanzania, Padri Francis Kangwa, unaendelea na kwamba atatoa taarifa pindi utakapokamilika. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Askofu Ruwa’ichi ametoa kauli hiyo leo tarehe 21 Aprili 2022, katika Kituo cha Hija cha Pugu wakati akiendesha misa ya mazishi ya mwili wa Padri Kangwa, uliokutwa kwenye tanki la maji la nyumba ya mapadri iliyopo jengo la Ottoman jijini Dar es Salaam, tarehe 15 Aprili mwaka huu.
Askofu Ruwa’ichi amesema hadi leo ibada ya mazishi ya Padri Kangwa inapofanyika, hawajapata taarifa kuhusu mazingira ya kifo chake.
“Na wale mnaododosa kwenye vyombo vya mitandao ya kijamii mtakumbuka kwamba, mwakilishi wa Jeshi la Polisi Dar es Salaam, alitoa taarifa ambayo ni tamko alituambia kwamba uchunguzi bado unaendelea. Nami naomba niwaambie hata leo tunapoenda kumzika Padri Francis hatujapata kauli ya mwisho kuhusu mazingira yote yaliyohusiana na kifo chake,” amesema Askofu Ruwa’ichi.
Kiongozi huyo wa kiroho ametoa kauli hiyo baada ya kuibuka maswali mengi juu ya chanzo cha kifo hicho, ambapo amesema kwa sasa hana maelezo ya kutoa kuhusu suala hilo.
“Wamejaribu kututafuta kwa maelezo na wale waliofaulu kunipata niliwaambia kwamba tunaelewa kilichotokea ni kizito, linafanyiwa kazi na vyombo husika na kwa hiyo kwa wakati huu sina maelezo. Nikiwa na maelezo ya kutoa basi nitawapa,” amesema Askofu Ruwa’ichi.
Askofu Ruwa’ichi amesema “hata hivyo, ndugu zangu nawaomba tukubali kwamba tunao msiba wenye changamoto, lakini pia tunao msiba ambao lazima tuukubali kama wakristo. Tuukabili kama wana wa Pasaka na kwa msingi huo nashukuru mliojitokeza kwa adhimisho hili la kumuombea na kumzika Padri Francis,” amesema.
Askofu Ruwa’ichi amewaomba waumini kumuombea Padri Kangwa kwa Mungu, ili apumzike kwa amani.
Ibada hiyo ya mazishi imehudhuriwa na watu mbalimbali, ikiwemo mapadri zaidi ya 50 na waumini wa Kanisa Katoliki kutoka maeneo mbalimbali.
Leave a comment