WATANZANIA wametakiwa kusherehekea Mapinduzi ya Zanzibari kwa kukumbuka kazi kubwa walizozifanya na waasisi wa Tanganyika na Zanzibar. Anaripoti Danson Kaijage Dodoma… (endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 12 Januari 2022 na Askofu Mkuu wa Kanisa la Maombi na Maombezi kwa Mataifa Yote (RUTACH), Living Mwambapa wakati akizungumzia sherehe za Mapinduzi hayo kilele chake kimefanyika katika Uwanja wa Amani Visiwani Zanzibar.
Amesema katika kusherehekea Mapinduzi hayo ni vyema zikaambatana na elimu ya historia ili kutoa mafundisho hususani kwa vijana ambao kwa sasa wanaibukia.
“Tunaposherekea sikukuu ya Mapinduzi tunatakiwa kutafakari mambo makubwa ambayo yamefanywa na waasisi wa Mapinduzi kwa kufanya Mapinduzi matukufu ya Zanzibari.
” Pia kuna haja ya kutoa elimu ya uraia kwa vijana ambao wanachipukia kwa nia thabiti ya kuwa wazalendo wakweli na kuipenda nchi yao na kuwatii viongozi” amesema Askofu Mwambapa.
Aidha, amesema kwa wakati uliopo, nchi inahitaji maombi na maombezi ya kweli ili kuhakikisha watumishi wa umma, wanasiasa na Serikali wanafanya kazi kwa umoja na kwa kujali maslahi mapana ya nchi na wananchi.
“Nawasihi viongozi wa dini kuwa na muda wa kutosha kuliombea Taifa pamoja na mihimili yote, Rais na jamii kwa ujumla sambamba na kusisitiza umoja, ushirikiano na kuitunza amani,” amesema Askofu Mwambapa.
Pia amewataka vijana na wale wasiokuwa na kazi kutokaa vijweni badala yake watafute fursa mbalimbali za kuweza kujipatia kipato
Leave a comment