Askofu Dk. Mwamakula, ameachiwa huru na jeshi hilo mchana huu wa Jumanne, tarehe 16 Februari 2021, baada ya kumfanyia upekuzi nyumbani kwake.
Kiongozi huyo wa kiroho na kijamii, alikamatwa jana Jumatatu, tarehe 15 Februari 2021, kufuatia madai yaliyotolewa na polisi kuwa alikuwa akihamasisha uhalifu.
Akizungumza na mwandishi wa habari, leo Jumanne, 16 Februari 2021, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa amesema, “baada ya kwenda kufanya upekuzi nyumbani kwake, mchana huu tumemuachia kwa dhamana baada ya kutimiza masharti,” amesema.
Kuachiwa kwake kwa dhamana kumejuka katika kipindi ambacho watu mbalimbali, pamoja na vyama vya siasa, kikiwamo ACT – Wazalendo, kutoa wito kwa jeshi hilo kumuachia huru Askofu Dk. Mwamakula.
Katika taarifa yake kwa umma, chama hicho kimesema, kinalaani kitendo cha kumkamata na kumshikilia Askofu Dk.Emmaus Mwamakula, kwa kuwa hakuna sheria yoyote aliyoivunja.
“Askofu Dk. Mwamakula amejitolea kuhamasisha kwa njia za amani, uwepo wa mabadiliko ya katiba ya nchi itakayotoa fursa ya kuundwa kwa Tume huru ya uchaguzi. Kwa msingi huo, mpaka hapo, hakuna kosa lolote ambalo Askofu amelifanya.
“Ibara ya 20(1) ya Katiba, inatoa haki kwa kila raia kuwa huru, kukutana na watu wengine kwa hiari yake na kwa amani, kuchanganyika na kushirikiana na watu wengine, kutoa mawazo hadharani,” imeeleza sehemu ya taarifa ya chama hicho kwa vyombo vya habari.
Naye Sheikh Ponda Issa Ponda, ambaye ni katibu wa Jumuiya na taasisi za Kiislamu ameeleza hatua ya kumkamata Askofu Dk. Mwamakula kuwa inalenga kuwatia hofu wananchi na hasa baadhi ya viongozi wa madhehebu ya kidini nchini.
Kwa mujibu wa Sheikh Ponda, kitendo cha kumkamata Askofu Dk. Mwamakula, kinaonyesha kuwa hali ya watetezi wa haki inavyozidi kuwa ngumu, na kwamba kumkamata kiongozi huyo kwa kuwa anaweka nia yake njema ya kulipatia taifa katiba mpya, ni muendelezo wa vitisho.
“Askofu Mwamakula kasema, yeye kwa maoni yake, anadhani kipaumbele chake kwa sasa, ni kurejewa katika kiporo cha katiba mpya. Ametaka kuwaunganisha watu katika kukumbusha mamlaka za serikali,” ameeleza.
Embu wataalamu wa sheria tunaomba mtufahamishe ivi huyu askofu amehalifu sheria gani? Je watetezi wa haki za binadamu nao wako wapi? Ndaga fijo