ASKOFU wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Mashariki na Pwani, Dk. Alex Malasusa, amesema Bara la Afrika halihitaji siasa peke yake, bali linahitaji uongozi kwa ajili ya kujiletea maendeleo yake. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Askofu Malasusa ameyasema hayo leo tarehe 2 Aprili 2021, wakati anazungumzia kifo cha aliyekuwa Rais wa Tanzania, Hayati Dk. John Magufuli.
Kwenye Ibada ya Kitaifa ya Ijumaa Kuu ya Pasaka, iliyofanyika katika Kanisa la Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Champlaincy Chuo Kikuu cha Dar es salaam (UDSM), mkoani Dar es Salaam.
Dk. Magufuli alifariki dunia akiwa madarakani tarehe 17 Machi 2021, kwa ugonjwa wa mfumo wa umeme wa moyo, katika Hospitali ya Mzena, Makumbusho mkoani Dar es Salaam, kisha nafasi yake ikachukuliwa na aliyekuwa Makamu wake wa Rais, Samia Suluhu Hassan.
“Afrika inahitaji kiongozi kwa ajili ya maendeleo, hatuhitaji siasa tu bali tunahitaji uongozi, ndicho tunacho-miss (kosa) Afrika , maneno yanakuwa mengi utedaji haupo,” amesema Askofu Malasusa.
Akimzungumzia Dk. Magufuli, Askofu Malasusa amesema, mwanasiasa huyo alikuwa fahari ya Waafrika, kwa kuwa aliweza kufanya vitu vingi ndani ya muda mfupi.
“Hayati Dk. John Magufuli alikuwa fahari ya Waafrika, kwamba kwa muda mfupi ameweza kufanya kitu ambacho labda kisingefanyika au kufanyika muda mrefu sana,” amesema Askofu Malasusa.
Askofu Malasusa amesema “Uongozi wa Magufuli ulikuwa wa kipekee nasi Watanzania tuna cha kujifunza.”
Safari ya miaka 61 ya Dk. Magufuli duniani ilihitimishwa tarehe 26 Machi 2021, baada ya mwili wake kuzikwa nyumbani kwao Chato mkoani Geita.
Akizungumzia mchakato wa Rais Samia kuapishwa kuwa Rais wa Tanzania baada ya Dk. Magufuli kufariki dunia, kufanyika kwa amani na utulivu, Askofu Malasusa amesema hatua hiyo inadhihirisha kwamba nchi imekomaa.
“Tunamshukuru Mungu kwa utulivu, sisi kama Watanzania katika kipindi hiki cha maombolezo . Nimpongeze sana rais wetu Mama Samia, kwa kupokea kazi hii lakini tujipongeze na sisi Watanzania kwa utulivu,” amesema Askofu Malasusa.
Askofu Malasusa ameongeza “ Mahali pengine si kitu kinatokea hivi hivi. Mungu amekuwa juu yetu, amekuwa juu ya Taifa hili, hata wasiotupenda nina hakika wakiwa peke yao wanasema hawa ni ukomavu na utulivu ambao umeendelea kuwepo.”
Rais Samia aliapishwa kuwa Rais wa Tanzania katika Ikulu ya Dar es Salaam, tarehe 19 Machi 2021.
Askofu Malasusa amewaomba Watanzania waendelee kumuombea Rais Samia, ili atekeleze majukumu yake kwa ufanisi kwa ajili ya kuijenga Tanzania.
Leave a comment