ASKOFU Mkuu, Jimbo Kuu la Katoliki Dodoma, Beatus Kinyaiya, amemtaja Rais Samia Suluhu Hassan kwamba ni kiongozi shupavu, mkakamavu, jasiri, mtenda haki, mwenye hekima na busara. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
“Rais huyu ni shupavu, mkakamavu, jasiri, mtenda haki, mwenye hekima na busara. Hii ni bahati kwa Tanzania kuwa na rais mwanamke katika Ukanda wa Afrika Mashariki,” amesema Askofu Kinnyaiya.
Askofu Kinyaiya ametoa kauli hiyo leo tarehe 11 Aprili 2021, wakati akizungumza kwenye ibada maalumu ya wamama wakatoliki Tanzania (WAWATA).
Katika mahubiri yake, amesema Mungu amempa heshima kubwa mwanamke kwa kuzingatia mambo mbalimbali.
Amesema, vigezo ambavyo Mungu aliviangalia kwa mwanamke ni pamoja na uaminifu, upendo, uthamini, utendaji wa kazi na nafasi ya mwanamke katika jamii.
Askofu Kinyaiya amesema, kwa kuzingatia vigezo hivyo, Mungu alimfanya mwanamke kuwa muhimu na ndiyo maana hata wakati wa siku ya kufufuka kwa Yesu, aliyetokewa wa kwanza na kupata habari alikuwa mwanamke.
Kiongozi huyo wa kiroho amesema, mwanamke anayo heshima ya kuheshimiwa na kusikilizwa, kwa kuwa Mungu kamthamini kwa kiwango cha juu.
Kutokana na hali hiyo, Askofu Kinyaiya amekemea watu wenye tabia ya kunyanysa wanawake, hasa wanaodhani wamewanunua wake zao.
Leave a comment