ASKOFU Josephat Gwajima, mgombea ubunge wa Kawe kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), amesifu miradi iliyotekelezwa jimboni humo kwa mwaka 2015 – 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Jimbo hilo la Kawe jijini Dar es Salaam, linaongozwa na Halima Mdee wa Chadema kwa miaka kumi mfululizo kuanzia (2010 – 2020). Mdee anatetea tena jimbo hilo katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.
Askofu Gwajima wa Kanisa la Ufufuo na Uzima amesema, miradi hiyo ikiwemo wa maji utafanya jimho hilo tatizo la maji kuwa historia.
Askofu Gwajima ametoa kauli hiyo leo Jumatano tarehe 14 Oktoba 2020, kwenye kampeni za urais za Dk. John Magufuli, mgombea urais wa Tanzania kupitia chama hicho katika viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe jijini Dar es Salaam.
Akizungumza mbele ya Dk. Magufuli, Askofu Gwajima ameeleza miradi mbalimbali iliyofanywa jimboni humo ikiwemo suala la elimu na fedha za mikopo kwa wananchi wa Kawe.
Askofu Gwajima amesema, lichja ya jimbo hilo kuongozwa na upinzani lakini Rais Magufuli alipeleka maendeleo “…lakini uliweka maendeleo kwa njia mbalimbali uliyoipata, zingine kupitia manispaa, zingine mkuu wa wilaya.”
“Kwa mfano, mradi wa maji, uliweka mradi wa maji katika Jimbo la Kawe wenye thamani ya Sh.74 bilioni ambao umetekelezwa katika Kata ya Mabwepande, Kata ya Wazo, Kata ya Mbezi Juu.”
“… na ukajenga matenki manne yenye ujazo wa mita milioni sita kila moja ambayo yatasambazwa kwenye urefu wa kilomita 1219, na hii sasa itafanya tatizo la maji Madale kuwa historia, tatizo la maji Kisanya kuwa historia, tatizo la maji kwenye Jimbo la Kawe itakuwa historia,’ amesema.
Kauli hiyo imepokewa kwa shwangwe na Mdee ambaye kwenye ukurasa wale wa twitter, ameeleza kushukuru ujio wa Dk. Maguifuli kwenye jimbo hilo akisema, “wamenifanyia kampeni nzuri sana leo…. Asante sana kwa kuja @MagufuliJP” “
Akizungumza na mtandao huu kuhusu shukrani hizo, Mdee amesema, Gwajima amesaidia kuwaeleza wakazi wa Kawe namna nilivyopigana ili kutatua kero ya maji.
“Utatuzi wa kero ya maji aliouzungumzia, umefanyika katika miaka hii mitano (2015 –2020), mimi nikiwa mbunge. amethibitisha kwamba, nimetekeleza wajibu wangu kwa wananchi na serikali iliwajibika katika hilo,” amesema Mdee.
Leave a comment