ASKOFU Mkuu wa Kanisa la Kiinjili na Kilutheri Tanzania (KKKT), Dk. Fredrick Shoo amesema amewashangaa na kuhuzunika kusikia baadhi ya viongozi wa kawaida na wa dini wanapowahamasisha watu kutofuata taratibu na hatua za kujikinga na ugonjwa wa UVIKO-19. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilimanjaro … (endelea).
Askofu Dk. Shoo ametoa kauli hiyo leo tarehe 16 Oktoba, 2021 katika ibada maalumu ya maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 ya Hospitali ya KCMC, Moshi mkoani Kilimanjaro.
Rais Samia ambaye yupo mkoani Kilimanjaro kwa ziara ya siku mbili, ameshiriki katika maadhimisho hayo na kufungua mnara wa jubilee hiyo.
Askofu Dk. Shoo amesema jambo hilo linasikitisha sana.
“Niliwashangaa sana na kweli nimehuzunika kusikia baadhi ya viongozi hata viongozi wa dini wanapowahamasisha watu kutofuata zile taratibu na hatua za kujikinga na ugonjwa wa UVIKO-19, inasikitisha.
“Rais umetuonesha njia, kwa hili nipende kukuambia tunakushukuru na tunakuunga mkono 100 kwa 100.
Pamoja na huduma ya afya ambayo serikali imeweka wazi kwamba imeipa kipaumbele kwa wananchi wa nchi hii,” Askofu Dk. Shoo.
Aidha, Askofu Dk. Shoo amemuomba Rais Samia kuendelea kushirikiana ili kuboresha huduma za afya nchini.
“Tunapenda kuzidi kukuomba kwamba vituo hivi ambavyo Mungu ameweka kwa kusudi lake la kurudishia afya watu wake tuendelee kushirikiana kwa pamoja, uendelee kutupatia msaada kama ambavyo serikali imekuwa ikifanya ili kuboresha huduma hizi,” amesema Askofu Dk. Shoo.
Leave a comment