ASKOFU wa Kanisa la Kiinjili la Kulutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Karagwe mkoani Kagera, Benson Bagonza amesema, ibada zilizositishwa ili kujikinga na maambukizo ya ugonjwa unaotokana na virusi vya corona (COVID-19) zitarejea tarehe 31 Mei, 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Tarehe 26 Aprili, 2020, Askofu Bagonza alitangaza kusitisha ibada na mikusanyiko yote akieleza sababu ya kufanya hivyo ni dayosisi hiyo kuwa mpakani na nchi ambazo raia wake wanatoroka na kuingia Tanzania.
Akizungumza na MwanaHALISI ONLINE leo Jumatano tarehe 20 Mei, 2020 iliyotaka kujua ibada hizo zitarejea lini, Askofu Bagonza amesema, Ibada hizo zilisitishwa kwa kipindi cha wiki nne ili kuweka mazingira sawa.
“Tuliunda kikosi kazi kupitia maeneo mbalimbali na kazi imekamilika na tarehe 31 Mei, 2020 ibada zinarejea,” amesema Askofu Bagoza.
Akitaja baadhi ya mambo iliyobaini kikosi hicho iliyopitia makanisa yote 267 ya Dayosisi hiyo ni, “kila kanisa ziwepo Ibada mbili kila Jumapili na watu watapangwa kila kitongoji kuingia kanisani.”
Askofu Bagonza amesema, kila muumini atakayefika kanisani, atapaswa kuvaa barakoa ambapo tayari wamenunua barakoa zaidi ya laki moja.
“Tumenunua ‘themo scaner’ kupima joto, vitakasa mikono, ndoo na kila kanisa vifaa vitakuwepo bila shida,” amesema kiongozi huyo wa kiroho.
Amesema, kikosi hiko, kimebaini baadhi ya makanisa yana madirisha madogo, hivyo wamekubaliana kuyapanua pamoja na kufanya upuliziaji, “hata kama watalamu wamesema haiui, ila tunajihakikishia tunakuwa salama zaidi.”
Askofu Bagonza amesema, “makatazo mengine yamewekwa, ibada zinakuwa fupi na washirika wanakaa kwa kuzingatia umbali ili wasibanane. Haya yote tusingeweza kuyafanya wakati watu wakiwa ndani, ndiyo maana tuliamua kusitisha ili kufanya maboresho.”
Leave a comment