SAKATA la wanachama 19 wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kwenda kinyume na msimamo wa chama hicho kwa kukubali uteuzi wa wabunge viti maalumu limesababishwa na mmomonyoko wa maadili. Anaripoti Regina Mkonde, Da es Salaam … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo Alhamisi tarehe 26 Novemba 2020 na Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Karagwe, Benson Bagonza, alipohojiwa na MwanaHALISI Online juu ya maoni yake kuhusu sakata hilo.
Sakata hilo liliibuka baada ya wanachama 19 wakiongozwa na Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha), Halima Mdee kuapishwa kuwa wabunge wa viti maalumu na Spika wa Bunge, Job Ndugai Jumanne ya tarehe 24 Novemba 2020.
Wanachama hao wanadaiwa kwenda kinyume na msimamo wa Chadema wa kutopeleka bungeni wawakilishi wake, wakipinga matokeo ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika tarehe 28 Oktoba 2020, kwa madai mchakato wake haukuwa huru na wa haki.
Alipouliza sababu za mgongano huo, Askofu Bagonza amesema Tanzania inakabiliwa na tatizo la mmomonyoko wa maadili, kwa kuwa watu wanaheshimu matokeo kuliko mchakato.
“Nadhani kuna mpalaganyiko wa kimaadili katika Taifa letu, kwamba mara nyingi tuna heshimu matokeo kuliko mchakato. Nchi yenye maadili ina heshimu michakato kuliko matokeo, nchi isiyo na maadili ina heshimu matokeo kuliko mchakato,” amesema Askofu Bagonza.
Kiongozi huyo wa kiroho amesema, wanachama hao wa Chadema waliokubali uteuzi ubunge viti maalumu wameheshimu matokeo badala ya mchakato uliotengeneza nafasi hizo.

“Penye maadili unahehsimu mchakato kuliko matokeo, pasipo na maadili unaheshimu matokeo, mchakato unauacha maadamu ufike unapokwenda, waliokubali uteuzi wa ubunge viti maalumu wameheshimu matokeo na si mchakato,” amesema Askofu Bagonza.
Kufuatia sintofahamu hiyo, Askofu Bagonza amekishauri Chadema kichukue hatua kwa wahusika bila kujali upendeleo.
“Tukio hili sio la kwanza kutokea katika historia ya nchi yetu, kwa hiyo, ningeshauri lishughulikiwe kama mengine yalivyoshughulikiwa yenye sura kama hii. Ili kuepusha mgongano wa kimaslahi,” amesema Askofu Bagonza.
Wito huo wa Bagonza umekuja siku moja baada ya Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika kuwaomba Watanzania kuishauri Kamati Kuu ya chama hicho, namna ya kulishughulikia suala hilo.
Akizungumza na wanahabari jana Jumatano, jijini Dar es Salaam, Mnyika aliwaomba wadau wa siasa na Watanzania kwa ujumla kupendekeza adhabu itakayofaa wanachama hao kulingana na kosa wlailolifanya.
Wanachama wanaotuhumiwa pamoja na Mdee kukiuka msimamo huo ni, Ester Bulaya na Esther Matiko.
Wengine ni, Katibu Mkuu wa Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha), Nusrat Hanje. Katibu Mkuu Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha), na Grace Tendega.
Makamu Mwenyekiti Bawacha, Hawa Mwaifunga. Naibu Katibu Mkuu Bawacha, Jesca Kishoa na Katibu Mwenezi Bawacha, Agnesta Lambat.
Mwenyekiti wa Chadema Mkoa Mtwara, Tunza Malapo. Ceciia Pareso. Asia Mwadin Mohamed. Felister Njau. Naghenjwa Kaboyoka. Sophia Mwakagenda. Kunti Majala. Stella Siyao.Salome Makamba. Anatropia Theonest na Conchesta Lwamlaza.
Wanachama hao wameitwa kujieleza mbele ya Kamati Kuu ya Chadema katika kikao chake kitakachofanyika kesho Ijumaa tarehe 27 Novemba 2020 jijini Dar es Salaam.
Sheria na kanuni za Chama zitumike bila kumuonea au kumpendelea mtu yeyote
Nina hamu ya kuelewa zaidi undani wa sakata hili hasa baada ya kumuina Mnyika akisema kwamba “hakusaini fomu za watu hao”. Nani yupo nyuma ya hili???✌