ASKOFU wa Dayosisi ya Karagwe, ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dk. Benson Bagonza, amesema Chama Cha Mapinduzi (CCM), kitakufa kwa sababu kinaamini hakitakufa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Iringa … (endelea).
Askofu Bagonza ametoa kauli hiyo leo Jumatatu, tarehe 8 Machi 2022, akihutubia kwenye kongamano la siku ya wanawake duniani, lililoandaliwa na Baraza la Wanawake la Chama cha Chadema (BAWACHA), mkoani Iringa.
“Imani ya kuwa CCM itatawala milele ni potofu, hakuna umilele wa chama chochote kilichoundwa na mwanadamu. CCM itakufa kwa sababu moja kuu, kwa sababu ina amini kwamba haitakufa. Yaani ukiamini hautakufa ndiyo utakufa. Tunaalikwa kupokea mabadiliko tusiyoyapenda katika maisha yetu,” amesema Askofu Bagonza.
Chama cha CCM kiliundwa 1977, baada ya Chama cha Tanganyika African National Union (TANU), kutoka Tanganyika, kwa sasa Tanzania Bara, kuungana na Afro-Shiraz Party, cha Zanzibar. CCM kimeitawala Tanzania tangu kuanzishwa kwake hadi sasa.
Askofu Bagonza amesema, tangu Awamu ya Kwanza ya Uongozi wa Tanzania, chini ya Rais Julius Kambarage Nyerere, Mungu amekuwa akiirudisha nchi kwenye mstari kila inapojaribu kupotea katika misingi yake.
“Tangu awamu ya kwanza ya uongozi wa Taifa letu, Taifa likielekea kupotea njia, Mungu analirudisha kwa aina ya pekee. Haimaanishi kwama mambo yetu hapa ndani safi, sio maana yangu bali Taifa letu linaishi kwa matumaini kwamba kesho itakuwa bora kuliko leo,’ amesema Askofu Bagonza.
Kiongozi huyo wa kidini amesema, mtu anayejaribu kuzuia kesho bora ya Tanzania, ajiandae kwa mshangao.
Wakati huo huo, Askofu Bagonza ameshauri mamlaka za Serikali kutenda haki, kwa kutunga sheria zisizokuwa kandamizi.
“Imani ya kwamba dhuruma na ukandamizaji vinalindwa na sheria kandamizi, ni potofu. Sikiliza kwa makini, sheria kandamizi hutengenezwa na watu wenye fikra za dhuruma na ukandamizizaji. Ni matokeo sio njia,” amesema Askofu Bagonza na kuongeza:
“Watu wenye fikra za dhuruma wanaunda sheria kandamizi, zisipofutwa hizi sheria zina tabia ya kuwatafuna waliozitunga. Tunaalikwa sote kutenda haki katika kutunga sheria, kwa sababu hatuna mamlaka juu ya kesho yetu.”
Leave a comment