ASKOFU wa Dayosisi ya Karagwe ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, KKKT, Dk. Benson Bagonza, amesema miaka kumi iliyopita alipingwa na baadhi ya wazee wa Tanzania, alivyopendekeza uteuzi wa mwanamke katika nafasi ya urais. Anaripoti Mwandishi Wetu, Iringa…(endelea).
Kiongozi huyo wa kidini ametoa ushuhuda huo leo Jumatatu, tarehe 8 Machi 2022, mkoani Iringa, alipokuwa anaelezea athari za mfumo dume, kwenye kongamano la maadhimisho ya siku ya mwanamke duniani, yaliyoandaliwa na Baraza la Wanawake la Chadema (BAWACHA).
“Miaka 10 iliyopita nilishiriki katika mazungumzo ya faragha na wazee wakubwa, wenye heshima katika Taifa hili. Wakati huo kulikuwa na mjadala ukiendelea juu ya nani anaweza kuwa Rais wetu. Wakati huo kulikuwa na majina matatu ya wanawake wakitajwa tajwa,” amesema Askofu Bagonza.
Askofu Bagonza amesema “nilipotoa mchango wangu kuunga mkono mojawapo ya jina hilo, hali ilibadilika katika mazungumzo yale. Wazee walinigeuka wakanisema na kusema wakati wa mwanamke kuwa Rais bado sana.”
Amesema wazee hao ambao hakuwataja jina, walimpinga juu ya pendekezo hilo, wakisema Urais una mambo mengi ya kiume.
“Nikawauliza kwa nini? Wakasema urais una mambo mengi ya kiume. Wakaorodhesha mambo siwezi kuyataja hapa. Lakini kwa ujumla wake ilikuwa kila kitu kinaanza na Rais kinamalizika na Rais. Ndugu znagu kina mama naomba mjue kiini cha ukandamizaji kinaanzia katika fikra zianzounda mifumo,”amesema Askofu Bagonza.
Akizungumzia kongamano hilo, Askofu Bagonza amesema amekubali kushiriki na BAWACHA kutokana na historia iliyotokea Tanzania, ya kuwa na Rais wa kwanza mwanamke, Samia Suluhu Hassan.
“Nimekubali kuongea nanyi kutokana na tukio la kihistoria katika Taifa letu, kwa mara ya kwanza tumempata Rais mwanamke na mwezi huu anaadhimisha mwaka mmoja tangu alipoingia madarakani,” amesema Askofu Bagonza na kuongeza:
“Nimeona nishiriki na ninyi kumshukuru Mungu kwa kutupatia funzo kwa njia ya ajabu, aliyewekwa kuwa mgombea mwenza pengine kwa kujaribiwa, sasa ni Rais wetu, tunamshukruu Mungu kwa jambo hili, mama yuko ofisini si kwa kupenda kwetu, bali kwa mapenzi ya Mungu.”
Rais Samia aliingia madarakani tarehe 19 Machi 2021, kufuatia kifo cha mtangulizi wake, Hayati John Magufuli, aliyefariki dunia tarehe 17 Machi mwaka jana, akipatiwa matibabu kwenye Hospitali ya Mzena, Makumbusho mkoani Dar es Salaam.
Kabla ya kuingia madarakani, Rais Samia alikuwa Makamu wa Rais wa Tanzania, ambaye alikuwa mgombea mwenza wa Hayati Magufuli, kwenye kinyang’anyiro cha Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika Uchaguzi Mkuu wa 2020.
Rais Samia amekuwa mwanamke wa kwanza Tanzania, kuvunja rekodi ya kuwa Makamu wa Rais (Novemba 2015 hadi Machi 2021) na Rais wa nchi hiyo kuanzia Machi 2021 hadi sasa.
Leave a comment