ASASI za kiraia (AZAKI) nchini Tanzania, zimeomba kukutana na Rais Samia Suluhu Hassan, kwa ajili ya kujadiliana nae masuala mbalimbali ikiwemo ufufuaji wa mchakato wa katiba mpya na ushirikiano baina yao na serikali yake. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Ombi hilo limetolewa leo Jumatatu tarehe 29 Machi 2021, wakati AZAKI hizo zinatoa tamko la kumpongeza Rais Samia.
Akitoa tamko hilo, Bob Wangwe, Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba Tanzania, amemuomba Rais Samia kutenga muda ili akutane nao.
“Tunamuomba Rais Samia kadri ratiba yake itakavyoruhu, tungepata kuonana nae ili kujadiliana nae masuala ya kitaifa ikiwemo katiba mpya na mashirikiano ya asasi za kiraia na Serikali yake,” amesema Wangwe.
Naye Mratibu wa Watetezi wa Mtandao wa Haki za Binadamu (THRDC), Onesmo Olengurumwa, amemuomba Rais Samia kuondoa sheria kandamizi katika ukuzaji misingi ya haki za binadamu na utawala bora.
“Tunaomba sheria zinazoweka mkinzano katika asasi za kiraia ziboreshwe, asasi zimepata mkwamo wa kufanya kazi zake kutokana na baadhi ya sheria kandamizi,” amesema Olengurumwa.
Ombi hilo la AZAKI kwa Rais Samia, limetolewa siku kadhaa baada ya kuapishwa kuwa Rais wa Tanzania, tarehe 19 Machi 2021, Ikulu jijini Dar es Salaam.
Rais Samia aliapishwa kurithi mikoba ya aliyekuwa Rais wa Tanzania, Hayati Dk. John Pombe Magufuli, aliyefariki dunia tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena, Makumbusho mkoani Dar es Salaam.
Dk. Magufuli alifariki dunia kutokana na matatizo ya mfumo wa umeme wa moyo, mwili wake ulizikwa nyumbani kwao Chato mkoani Geita, Ijumaa ya tarehe 26 Machi 2021
Leave a comment