KLABU ya Arsenal inayoshiriki Ligi Kuu England imewatandika Mashetani Wekundu ‘Manchester United’ jumla ya bao 3- 2 katika mchezo uliopigwa leo jijini London nchini Uingereza. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mtanange huo uliopigwa leo tarehe 22 Januari, 2023 katika dimba la Emirates umeshuhudiwa washika bunduki hao wa London wakiendelea kujikita kileleni kwa kuwa na pointi 50.
Mashetani hao walikuwa wa kwanza kupata bao dakika ya 17 na Marcus Rashford baada ya kuachia shuto kali katikati ya mabeki wa Arsenal na kuelekea upande wa kulia na kumshinda kipa wa Arsenal Aaron Ramsdale.
Hata hivyo, Arsenal walijibu mapigo dakika saba baadae ambapo Mshambuliaji hatari wa Arsenal, Eddier Nketiah kwa kichwa baada ya kupokea krosi safi ya Granit Xhaka.
Kipindi cha kwanza kilikatika kwa wababe hao kuenda kwenye vyumba vya mapumziko wakiwa wametoshana kwa bao 1-1.
Aidha, Arsenal ambao waliendelea kuvamia lango la Mashetani kama nyuki katika kipindi cha pili walipata bao la pili dakika 53 kupitia kwa winga wao matata Bukayo Saka ambaye aliwahadaa mabeki wa Mashetani katika eneo la 18 na kuachia shuti kali lilioelekea lango lwa Man U upande kulia na kumshinda kipa David De Gea ambaye aliogelea bila mafanikio.
Manchester United walisawazisha goli hilo baada ya kipa wa Arsenal kutema mpira wa kona ambapo beki Lisandro Martinez alipiga kichwa cha kuchupa na kujaa wavuni.
Goli hilo liliiamsha Arsenal ambao walionesha mpira wa kuvutia na kulisakama lango la Mashetani hao hadi dakika ya 90 ambapo Nketiah aliunganisha pasi ya ‘Pass master’ Oleksandr Zinchenko raia wa Ukraine na kutupia goli la ushindi kwa washika bunduki hao.
Kwa matokeo hayo Arsenal wamefikisha pointi 50 na kujichimbia kileleni huku Manchester City wakifuatia kwa pointi 45 lakini wakiwa na mecho 20 mkononi wakati Arsenal wana mechi 19.
Mashetani wekundu ambao morali ya ushindi wa mechi kadhaa wamebaki na poonti 39.
Leave a comment