RAFU, hujuma na hila vimeanza kuchipuka, ambapo baadhi ya wagombea kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), wamedaiwa kunyimwa fomu kwa kutochangia mbio za Mwenge. Anaripoti Martin Kamote … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 29 Oktoba 2019, John Mrema ambaye ni Mkurugenzi wa Itikadi na Uenezi wa Chadema amesema, tayari hujuma zimeanza kwa baadhi ya wagombea wao kunyimwa fomu huku wengine wakikataliwa kupewa nakala baada ya kujaza fomu kama utaratibu unavyoelekeza.
“Kitongoji cha Ileje mkoani Songwe, mgombea wetu Joseph Mlagu amenyimwa fumo kwa madai kuwa hajatoa mchango wa Mwenge,” amesema Mrema na kuongeza;
“Kata ya Mboliboli mkoani Iringa, wagombea wamechukua fomu leo na wamejaza na kurejesha leo lakini msimamizi amekataa kuwapa nakala za fumo wakati kanuni zinasema, nakala inabaki kwa msimamizi nyingine kwa mgombea. Ni wazi kuwa baadaye wanataka wakatae kuwa hajapokea fumo hizo.”
Mrema amesema, chama hicho kimekuwa kikifuatilia taarifa za wagombea wake nchi nzima na kwamba, taarifa zimekuwa zikipokewa kila wakati.
“Hapa tunapokea taarifa kutoka maeneo yote ya nchi, tunakesha kujua nini kimefanyika wapi. Taarifa zingine zinaumiza, eti mtu ananyimwa fomu kwa kuwa hajachangia mchango wa mbio za mwenge,” amesema.
Ofisa huyo wa Chadema amesema, maeneo mbalimbali ya nchi taarifa zake zinaashiria mazingira yenye kutia shaka.
Amesema, Mkoa wa Songwe wasimamizi wa uchaguzi wametoa taarifa kwamba, miongoni mwa vyama ambavyo tayari vimechukua fomu ni pamoja jambo ambalo si kweli.
“Kata ya Illo wagombea wa Chadema hawajapewa fumo na walikuwa kwenye ofisi za wasimamizi tangu saa 12 asubuhi,” amesema na kuongeza “Chadema imeweka wasimamizi kusimamia watu watakaowatambulisha wagombea wao ili kuepuka kuhujumiwa.”
Akizungumzia Wilaya ya Karatu, Manyara Mrema amesema, wagombea wake wamewekewa mtego kwa kukabidhiwa nembo isiyo na nenmbo ya Halmashauri ya Wilaya ya Karatu.
“Wamekuwa wakiweka mitego mbalimbali, sasa unampa mgombea fomu isiyo na nembo, unataka baadaye uikatae ili CCM wapiti bila kupingwa sio?” amehoji.
Akizungumzia mkoani Rukwa amesema, Kata ya Kapenta msimamizi wa uchaguzi amegoma kutoa fomu kwa madai, mgombea wa Chadema hajatambulishwa kwake.
Leave a comment