JESHI la Polisi, Kanda Maalum ya Dar es Salaam limemkamata Wilfred Welandumi kwa madai ya kutumia jina la Dk. Bashiru Ally, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kufanya utapeli. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Akizungumza na Waandishi wa Habari leo tarehe 5 Aprili 2019, SACP Lazoro Mambosasa, Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam amesema, jeshi hilo limemwanika Welandumi (40) ili kuwapa wananchi tahadhari.
Kamanda Mambosasa amesema, Welandumi ni mkazi wa Yombo, Dar es Salaam.
“Mtuhumiwa huyo amekuwa akiwapigia simu baadhi ya wabunge wa chama tawala na kuwaomba fedha kwa kujifanya yeye ni Dk. Bashiru na hatimaye kufanikiwa kutapeli fedha kiasi cha Tsh. 370,000,” amesema.
Na kwamba, mtuhumiwa huyo hakutumia jina la Dk Bashiru pekee yake bali hata jina Prof. Makame Mbarawa ambaye sasa ni Waziri wa Maji.
Mtuhumiwa huyo atafikishwa mahakamani upelelezi utakapokamilika.
Leave a comment