WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni, amesema Jeshi la Polisi mkoani Geita, linamshikiria mtu mmoja kwa tuhuma za kumbaka mtoto wa miezi sita, akijaribisha dawa ya kuongeza nguvu za kiume. Anaripoti Mwandishi Wetu, Geita … (endelea).
Mhandisi Masauni ametoa kisa hicho, leo Jumatano, tarehe 8 Juni 2022, katika mkutano wa Rais Samia Suluhu Hassan na wananchi wa kata ya Bwanga, mkoani Gieta, akielezea mikakati inayofanywa na Serikali kuimarisha hali ya ulinzi na usalama.
“Leo nimejaribu kuzungumza na makamanda wa eneo hili, wakaniambia jana kulikuwa na taarifa ya mtu amembaka mtoto wa miezi sita, ni kitu ambacho cha kinyama kinasikitisha. Alipokamatwa na Polisi alipoulizwa akasema alikwenda kwa mganga akapewa dawa za kuongeza nguvu za kiume akaona ajaribie kwa mtoto,” amesema Mhandisi Masauni.
Mhandisi Masauni amesema,“ni jambo la ajabu la kusikitisha lenye kufedhehesha na halikubaliki.”
Kufuatia matukio hayo, Mhandisi Masauni amewaomba wananchi wawaripoti katika mamlaka za Serikali, Waganga wa kienyeji wanaohamasisha matukio ya ukatili wa kijinsia kwa watoto ikiwemo ubakaji na ulawiti.
“Napenda kutoa wito kwa wananchi kutoa ushirikiano kwa mifumo ya kiserikali ikiwemo askari kata, kubaini wanaofanya vitu vya ovyo kabla hawajatoa madhara ikiwemo hawa Waganga wanaosababisha vitu hivi vya ajabu katika nchi yetu kubwa,” amesema Mhandisi Masauni.
Waziri huyo wa mambo ya ndani ya nchi, amesema Serikali ya Rais Samia ameajiri Askari wakaguzi zaidi ya 6,000 waliopelekwa katika kata mbalimbali nchini kwa ajili ya kuimarisha ulinzi na usalama, ambapo amewataka wananchi kuwapa taarifa za uhalifu ili zifanyiwe kazi kabla ya haujaleta madhara.
Leave a comment