MASTEN Wanjala mtuhumiwa aliyegonga vichwa vya habari nchini Kenya baada ya kukiri kuwaua zaidi ya watoto 13 na baadaye kutoroka katika kituo cha polisi alipokua anazuiliwa, ameuawa na wananchi wa Bungoma Magharibi mwa Kenya. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Naibu Kamishena wa Kaunti ya Bungoma, Cornelius Nyaribai amethibitisha kifo chake katika ujumbe wa Twitter.
Polisi wanasema Wanjala alifuatwa na wanakijiji hadi nyumbani alipokuwa katika Mji wa Bungoma na kupigwa hadi kuondoa uhai wake.
“Kuna watoto waliokuwa wanaenda shule walimuona na wakamtambua na wakatoa taarifa Polisi, alikimbilia kwenye nyumba moja akajifungia, wananchi waliokuwa na hasira walivunja mlango na wakamtoa nje and within two seconds walikuwa wamemuua tayari”
Mamlaka za usalama nchini humo zilikuwa zimeanzisha msako mkali kumtafuta mtu huyo ambaye alikiri kuwaua zaidi ya wavulana kumi katika kipindi cha miaka mitano.
Tarehe 12 Oktoba mwaka huu, Masten Wanjala alitoroka katika mahabusu ya Kituo cha Polisi Jogoo jijini Nairobi saa chache kabla ya kuitikia mashtaka ya mauaji ya wavulana 13.
Hata hivyo, alikuwa anatarajiwa kupandishwa kizimbani tarehe 13 Oktoba, mwaka huu katika mahakama ya Madaraka.
Maofisa watatu wa Polisi wa Kenya waliokuwa kazini siku aliyotoroka mtuhumiwa huyo, walifikishwa mahakamani kwa tuhuma za kumsaidia mtuhumiwa huyo kutoroka.
Wanjala aliyekuwa na umri wa miaka 20, alikamatwa Julai mwaka huu kwa tuhuma za kufanya mauaji hayo mwaka 2019 na 2020.
Aidha, kijana huyo alikiri kutumia dawa za kulevya na kuwaua wavulana wadogo, na kunywa damu zao katika visa vingine.
Leave a comment