TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), inamshikilia aliyekuwa Mtendaji Mkuu wa Bohari ya Dawa (MSD), Laurean Bwanakunu na Kaimu mkurugenzi wa Lojistiki wa MSD, Byekwaso Tabura kwa tuhuma za rushwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea)
Taarifa iliyotolewa leo Jumanne tarehe 2 Juni 2020 na Afisa Uhusiano wa Takukuru, Doreen Kapwani imesema, Bwanakunu na Tabura wako mahabusu katika ofisi za taasisi hiyo Upanga jijini Dar es salaam kuanzia leo.
“Watuhumiwa hawa, wanakabiliwa na tuhuma kuhusu matumizi mabaya ya madaraka pamoja na kuisababishia Serikali hasara-kinyume na Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na.11 ya Mwaka 2007,” amesema Doreen.
Takukuru wamechukua uamuzi huo ikiwa zimepita siku 30 tangu Rais John Pombe Magufuli kumteua Brigedia Jenerali Dk. Gabriel Sauli Mhidize kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa (MSD).
Tarehe 3 Mei 2020, Rais Magufuli alifanya mabadiliko hayo ndani ya MSD na kumteua Dk. Mhidize ambaye alikuwa Mkuu wa Hospitali ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) Lugalo Jijini Dar es Salaam.
Hadi anatenguliwa, Bwanakunu alikuwa ameiongoza MSD kwa miaka minne na miezi tisa kuanzia tarehe 6 Juni 2015 alipoteliwa na Rais mstaafu Jakaya Kikwete kuongoza taasisi hiyo hadi tarehe 3 Mei 2020 alipotenguliwa.
Kabla ya uteuzi huo, Bwanakunu alikuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Ariel Glaser Paediatric AIDS Healthcare Initiative.
Leave a comment