MAKAMU wa Rais wa Tanzania mteule, Dk. Phillip Mpango, ameahidi kulitoa Taifa katika uchumi wa kati hadi uchumi wa juu katika kipindi cha muda mfupi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Dk. Mpango ametoa ahadi hiyo leo Jumanne tarehe 30 Machi 2021, baada ya Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kulipendekeza jina lake kuwa makamu wa rais, bungeni jijini Dodoma.
Akizungumzia mikakati yake katika kumsaidia Rais Samia, amesema Tanzania kuingia uchumi wa juu inawezekana, kama Serikali na Watanzania watashirikiana kwa pamoja.
“Nimesema mara kadhaa humu ndani (bungeni) tutoke low middle income tax (uchumi wa chini wa kati) twende high income tax (uchumi wa juu) katika kipindi kifupi na inawezekana kwa pamoja tukiamua kama Watanzania,” ameahidi Dk. Mpango.
Waziri huyo wa fedha na mipango amesema, katika majukumu yake mapya atasimamia haki za Watanzania wanyonge, kwa kuhakikisha wanapata huduma za muhimu.
“Nadhani nimejieleza mimi mwenyewe nilikotoka ni mtoto wa masikini kabisa, kama kiatu cha umasikini najua kinavyouma, kama mtanithibitisha hilo nawaahidi kuendeea kusimamia haki za wanyonge wa Tanzania,” amesema Dk. Mpango.
Mwanasiasa huyo ameahidi kumuenzi aliyekuwa Rais wa Tanzania, Hayati Dk. John Magufuli kwa kusimamia rasilimali za nchi, maadili ya watumishi wa umma na kuibadilisha Tanzania
“Jambo muhimu sana tunaloweza kumtendea haki Dk. Magufuli ni kuishi ndoto yake, lazima tuibadilishe Tanzania, lazima tusimamie rasilimali za nchi yetu, lazima tuhakikishe viongozi wote wa umma wanaishi maadili ya kazi waliyotumwa na Watanzania,” amesema Dk. Mpango.
Dk. Magufuli alifariki dunia akiwa madarakani, tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena, Makumbusho mkoani Dar es Salaam, alipokuwa anatibiwa ugonjwa wa mfumo wa umeme wa moyo.
Dk. Mpango amesema, katika uongozi wake hatowafumbia macho wanaoendekeza undugu kazini.

“Mjomba alikuwa zamani, lazima tusimamie rasilimali za nchi jicho lote hapo, kwa nafasi ya bunge katika hili ni muhimu sana, endapo bunge hili litanithibitisha katika nbafasi ambayo nimependekezwa ahadi yangu ni hiyo lazima tumuenzi rais wetu, lazima tutende wajibu wetu kwa Taifa hili,” amesema Dk. Mpango.
Mbunge huyo wa Buhigwe mkoani Kigoma, amependekezwa kumrithi Mama Samia, bada ya mwanamama huyo kuapishwa kuwa Rais wa Tanzania tarehe 19 Machi 2021, Ikulu jijini Dar es Salaam.
Mama Samia alikuwa Makamu wa Rais kwa miaka mitano na miezi mitano mfululizo (Novemba 2015 hadi Machi 2021), hadi Dk. Magufuli alipofariki dunia.
Mwili wa Dk. Magufuli ulizikwa nyumbani kwake Chato mkoani Geita.
Leave a comment