WAZIRI wa Elimu na Mafunzo, Prof. Joyce Ndalichako amesutwa na wanafunzi wa Chuo cha Usafirishaji Tanzania (NIT) baada ya kutaka kuwatetea wauaji wa Akwilina Akwilini. Anaripoti Mwandishi Wetu …. (endelea).
Tukio hilo limetokea leo Alhamisi Viwanja vya NIT, Mabibo jijini Dar es salaam wakati wa kuaga mwili wa Marehemu Akwilina, aliyeuwawa kwa risasi “iliyorushwa na Polisi” Ijumaa iliyopita wakati wa wafuasia wa Chadema walipokuwa wakielekea kwenye ofisi za Msimamizi wa Uchaguzi Kinondoni kudai fomu za viapo.
MwanaHALISI Online imeshuhudia wanafunzi hao wakinyanyua mabango yanayoashiria kutokukubaliana na utetezi uliokuwa ukitolewa na Prof. Ndalichako kwa niaba ya serikali kuhusiana na kifo cha Akwilini ambaye ni mwanafunzi wa mwaka wa kwanza katika mchuo cha NIT.
Aliyehamsha hisia kali za wanafunzi hao, alikuwa Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam pale alipodai kuwa kifo hakizuiliki na hivyo siku za kuishi za Akwilina duniani zilikuwa zimekwisha.
Maneno hayo ambayo yalionekana kuwakera wanafunzi waliokuwepo viwanjano hapo kwa lengo la kumuaga mwanafunzi mwenzao na kuanza kuibua minong’ono ya chinichini lakini hawajafanya lolote, Makonda alimkaribisha Prof. Ndalichako kuzungumza.
Prof. Ndalichako alipoanza hotuba yake kulikuwa na utulivu, lakini alitoa kauli ambazo zilikuwa zinaashiria kuwatetea wauaji wa Akwilina, ndipo alipojikuta yupo katikati ya mabango ya wanafunzi hao na kusababisha waombolezaji kuacha kusikiliza anachozungumza na kuangalia kilichoandikwa kwenye mabango hayo.
Wanafunzi walisimama kuonesha mabango yao kwa waandishi wa habari na miongoni mwa ujumbe uliokuwemo kwenye mabango hayo ni ule uliosema, “Tunataka tume huru ya uchunguzi” na mwingine ulisomeka, “Wauaji hawawezi kujichunguza.”
Mbali na mabango hayo ya wanafunzi, lakini Padre aliyekuwa akiongoza misa ya kumuaga marehemu Akwilina, Padre Raymond Mayanga wa Katisa Katoliki Parokia ya Yohana Mbatizaji Mabibo Luhanga, amepigilia msumari baada ya kusema serikali iache ujanja ujanja imtafute aliyempiga risasi iliyosababisha kifo cha Akwilina.
Amesema: “Serikali iache ujanja ujanja. Hiki siyo kipindi cha ujanja ujanja. Hiki ni kipindi cha kufanya toba. Serikali imtafute aliyempiga risasi Akwilina na aombe radhi kwa umma kupitia televisheni.”
Mbali na Akwilina watu wengine kadhaa walijeuruhiwa na risasi na kulazwa katika hospitali mbalimbali ikiwemo Mwananyamala na Muhimbili.
Leave a comment